// Disable text selection (not fully reliable) function disableSelection(element) { element.setAttribute('unselectable', 'on'); element.style.userSelect = 'none'; element.style.MozUserSelect = 'none'; element.style.webkitUserSelect = 'none'; } // Apply to the entire document body document.addEventListener('DOMContentLoaded', function() { disableSelection(document.body); }); MAKOCHA WAZUNGU WAMEKUJA KUUA SOKA YETU, AU NINI? - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE MAKOCHA WAZUNGU WAMEKUJA KUUA SOKA YETU, AU NINI? - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE
  • HABARI MPYA

    Sunday, December 13, 2015

    MAKOCHA WAZUNGU WAMEKUJA KUUA SOKA YETU, AU NINI?

    MIAKA ya karibuni limekuwa jambo la kawaida sana klabu kubwa nchini, Azam FC, Simba na Yanga SC kuwa chini ya makocha wa kigeni.
    Na bila shaka uamuzi wa kutumia makocha wa kigeni ni waje kusaidia kuinua viwango vya timu, baada ya kushindikana chini ya makocha wazawa.
    Enzi za makocha wazawa kufundisha klabu kubwa za Tanzania zilizikwa rasmi muongo uliopita na sasa wageni wanapishana kwenye mabenchi ya ufundi ya timu hizo.
    Azam FC kwa sasa ipo chini ya Muingereza Stewart John Hall, ambaye wasaidizi wake wote ni wageni, ukiondoa Dennis Kitambi na kocha wa makipa ni Iddi Abubakar.
    Simba SC ipo chini ya Muingereza pia, Dylan Kerr ambaye anasaidiwa na Mkenya, Abdul Iddi Salim baada ya kuondoka kwa Suleiman Matola.

    Yanga SC ipo chini ya Mholanzi, Hans van der Pluijm anayesaidiwa na mzalendo Juma Mwambusi, baada ya kuondoka kwa Charles Boniface Mkwasa.
    Kati ya makocha wote hao wa kigeni, angalau ni Stewart Hall pekee ameonekana kuwa na tija kwa soka ya Tanzania kutokana na dhamira yake halisi ya kukuza vipaji vya wachezaji wa nyumbani.
    Tunaona Stewart anavyowapa nafasi wachezaji wazawa katika kikosi chake na ndiyo maana kila baada ya muda anaibua vipaji vipya.
    Leo kinda Farid Mussa ni gumzo, hiyo ni kwa sababu ya sera za Stewart kuwapa nafasi wazawa – lakini amekuwa akisaidia kulinda vipaji vya wengine kama John Bocco, Aggrey Morris, Erasto Nyoni, Salum Abubakar na Himid Mao.
    Wote Bocco, Himid, Erasto, Morris na Sure Boy ni wachezaji ambao kwa hakika wangekuwa Simba au Yanga, sasa nao labda wapo Mwadui FC ya Jamhuri Kihwelo wanamalizia soka yao, lakini mbele ya Stewart bado wana thamani. 
    Tumekuwa na bahati mbaya sana katika soka yetu hatupati viongozi ama weledi, au wenye nia ya dhati ya kusaidia mpira wa nchi hii matokeo yake ile dhamira ya kuinua soka yetu, utekelezaji wake unakuwa mgumu.
    Tuna viongozi wasomi wa viwango vya juu, lakini ‘upumbavu’ wanaofanya huwezi kuona mwelekeo wa klabu. Ni watu ambao wanaonekana kama wapo kwa maslahi yao binafsi ni si klabu wala soka yetu.
    Kwa mtu yeyote mwenye akili zake timamu, lazima ataelewa dhana ya awali ya kuachana na makocha wazawa na kuhamia kwa makocha wa kigeni ilikuwa ni waje kusaidia kuinua uwezo wa wachezaji wetu na timu zetu.
    Wacheaji wetu wana mapungufu ya aina mbili tu, hawana mazoezi ya kutosha na pia wanapungukiwa maarifa – tulitarajia tutapata makocha wa kigeni watakaowaongezea hayo.
    Badala yake viongozi wasomi wameongoza dhana ‘hawafundishiki’ na sasa wanashirikiana na makocha hao wa kigeni kuhakikisha idadi ya wachezaji wa kigeni inaongezeka kila kukicha.
    Najiuliza hawa viongozi wa sasa walikuwa wapi enzi zile, makocha wa kigeni kutoka nchi jirani tu waliposaidia kuinua viwango vya wachezaji wetu, hadi nasi tukakiri ‘wamebadilika’?
    Nzoyisaba Tauzany ‘Bundesi’, sasa marehemu alikuja Yanga SC mwaka 1993 akitokea kwao Burundi na kukuta beki wa kulia ni mkongwe David Mwakalebela ‘MP’.
    Lakini baada ya kumtumia katika mchezo mmoja tu wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati mjini Kampala, Uganda dhidi ya SC Villa akiwa ‘uchochoro’ timu ikifungwa 3-0 hakumtumia tena, lakini hakuleta beki mgeni.
    Alimchukua kiungo Mtwa Kihwelo akamtayarisha kucheza beki ya kulia na akacheza hadi mwisho wa mashindano, timu ikitwaa Kombe na kurejea nalo Dar es Salaam, tena katika fainali ikiwafunga hao hao Villa 2-1. 
    Alifika kwenye mashindano Uganda, akaambiwa beki namba tano Salum Kabunda amegoma – Tauzany akaumiza kichwa akamchezesha marehemu Issa Athumani Mgaya sentahafu mwanzo hadi mwisho.
    Wengi watakumbuka Joseph Kaniki aliingia Simba SC mwaka 2000 kutoka Kariakoo United ya Lindi akiwa mchezaji mwenye mapungufu mengi na staili yake ya uchezaji kwa kiasi kikubwa ilikuwa kichekesho – silaha yake kubwa ilikuwa mashuti tu.
    Lakini alikuwa kocha Mkenya, James Aggrey Siang’a aliyembadilisha mchezaji huyu akawa bora zaidi na kuisaidia mno klabu hiyo.
    Tauzany pia akiwa Simba SC, alibadilisha mno uchezaji wa Athumani Machuppa na kumfanya atulize akili uwanjani badala ya kucheza kwa ajili ya kuwafurahisha mashabiki- na kweli akawa mshambuliaji tishio hapa nchini wakati wake.
    Wachezaji wa Tanzania miaka ya nyuma walikuwa wanaheshimika hadi nchi jirani Kenya na Uganda, lakini leo hali imebadilika.
    Hatukuweza kutoa wachezaji wa kucheza Ulaya, lakini tulitoa watu wa kwenda kucheza Uarabuni hususan Oman na wengi wamefanikiwa kubadilisha maisha yao kwa kucheza huko – leo Mtanzania gani anapata nafasi Uarabuni?
    Tumejiua. Tumejiua kwa kuendekeza kualika wachezaji wa kigeni waje kuitawala soka yetu.
    Na hii maana yake, tunaajiri makocha kwa gharama kubwa, lakini hawataki kufanya ngumu. Hawataki kuinua uwezo wa wachezaji wetu, zaidi ya kuletewa wachezaji ambao tayari wana uwezo mkubwa wazisaidie timu.
    Wachezaji wetu hawana nguvu na stamina kwa sababu ya lishe duni na mazoezi haba. Wanakosa maarifa ya kisoka, kwa sababu ya kutoibukia katika misingi mizuri ya soka kisoka.
    Je, baada ya makocha wa kigeni kuajiriwa katika klabu zetu huwa wanafanya nini kuwaongezea nguvu na stamina pamoja na maarifa ya kisoka wachezaji wetu?
    Staili yote na aina ya mazoezi wanayopewa Yanga sasa ni ile ile ya enzi za kocha Tarzan Kessy (marehemu) – wachezaji kukimbizwa raundi nyingi na kurushwa vihunzi, ikitokea wameenda gym mara moja kwa msimu.
    Aina ya lishe za wachezaji wa Simba SC kwa sasa bado zile zile za enzi za kocha Mohammed Kajole (marehemu), unatarajia mwili wa Said Ndemla utabadilika na kuwa kama wa Mbwana Samatta?
    Na kwa mtaji huo, hawa makocha wa kigeni wataendelea tu kutamani wachezaji wa kigeni. Na kwa bahati mbaya, hata hao wageni wakija nchini, chini ya Wazungu hao uwezo wao unaporomoka kutokana na kutopata mazoezi ya kiwango sahihi.
    Tuliona kwa Kpah Sherman wakati anakuja nchini alionekana yuko fiti kisawasawa, lakini baada ya muda akawa kama Jerry Tegete tu, kwa sababu msingi wa mazoezi uliomkuza siyo aliokutana nao Yanga.   
    Simon Msuva anamaliza msimu uliopita wa Ligi Kuu akiwa mfungaji bora akapata nafasi ya majaribio Afrika Kusini na kule alishindwa vitu vile vile ambavyo sote tunajua – kutokuwa fiti kwa asilimia 100 na maarifa haba ya kisoka. 
    Lakini leo kocha wa Yanga SC badala ya kufikiria kukuza uwezo wa Msuva, anatafuta winga kutoka Afrika Magharibi.
    Mrisho Ngassa alipokwenda West Ham United mwaka 2007 pamoja na kumvutia kocha Gianfranco Zola wakati huo, lakini akaambiwa arudi Afrika kuongeza lishe. Na hayo ndiyo matatizo yetu na sote tunafahamu kiasi gani TP Mazembe imetusaidia kukuza uwezo wa Samatta na Thomas Ulimwengu.
    Amini nakuambia, Samatta angebaki Simba SC kwa miaka hii tu minne sasa hivi angekuwa labda Mtibwa Sugar kwa Mekcy Mexime. 
    Leo imefikia Tanzania tunaletewa mawinga kutoka Niger, wakati nchi hii ilikuwa inaheshimika kwa wachezaji wa pembeni ukanda wote huu tangu enzi za akina Abbas Dilunga na Leonard Chitete kabla ya akina Sunday Juma, Abubakar Salum ‘Sure Boy’ (baba wa huyu anayecheza Azam sasa), Alfred Kategile na Edibily Lunyamila.
    Msingi wa soka ya vijana upo Azam FC tu, lakini huko Simba na Yanga ni ujanja tu halafu bado unaambiwa eti klabu na kiongozi anaitwa ‘Msomi’ wakati mambo yanaendeshwa kama Toroli All Star.
    Klabu haina Uwanja inasajili mchezaji mmoja kwa Sh Milioni 200. Klabu ina jengo, wanalala mchwa tu na mbu, wachezaji wanakwenda kupangiwa gesti jirani.
    Bado kiongozi kila siku anawasilisha kwa Mwenyekiti wazo la kusajiliwa mchezaji mpya wa kigeni kwa fedha ambazo ni bajeti ya mwaka ya Ndanda FC ya Mtwara.
    Wakati umefika sasa Watanzania tuamke na tuwashinikize makocha wa kigeni wafanye kazi ya kuinua uwezo wa wachezaji wetu na si kutaka kula fedha zetu kiulaini.
    Wachezaji wetu wanaweza, isipokuwa wana mapungufu kidogo tu, ambayo wakipatikana walimu weledi kweli kwenye klabu zetu watabadilika.
    Ziko wapi zile enzi kocha Tambwe Leya (marehemu) anawafundisha wachezaji wa Yanga SC darasani, uwanjani baada ya kuwajenga kwa mazoezi magumu kwenye miti ya miembe na ufukweni?
    Na hapo ndipo ninapojiuliza, makocha hawa Wazungu wamekuja kuisaidia, au kuiua soka yetu? Jumapili njema. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAKOCHA WAZUNGU WAMEKUJA KUUA SOKA YETU, AU NINI? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top