• HABARI MPYA

        Wednesday, October 23, 2013

        MALINZI AZINDUA KAMPENI ZA KURITHI KITI CHA TENGA TFF LEO, AAHIDI MAMBO MAKUBWA SOKA YA TANZANIA

        Mgombea Urais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Emil Malinzi akizungumza Waandishi wa Habari katika uzinduzi wa kampeni zake kuelekea uchaguzi Mkuu wa shirikisho hilo.
        "Ndugu zangu,
        Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema aliyetulinda na kutuwezesha kufika
        hapa tulipo.
        Tarehe 19 Novemba 2009 Rais Jakaya Mrisho Kikwete wakati anazindua ziara ya Kombe la FIFA la
        dunia uwanja wa Taifa, Dar Es Salaam pamoja na mambo mengine alisema, namnukuu:
        ‘‘Kwa Watanzania wenzangu tuichukulie ziara ya Kombe la Dunia nchini mwetu
        kama ni changamoto kubwa kwetu inayotutaka tufanye vizuri zaidi katika soka ili
        tulingane na heshima hii tuliyopewa. Hasa ni changamoto kwa viongozi wa soka wa
        ngazi zote pamoja na wachezaji na wapenzi wa mpira wa miguu nchini. Kuja kwa
        kombe hili ni deni kwetu na kulilipa kwetu sisi ni kuzinduka, tuendeleze kiwango
        chetu cha soka nchini ili na sisi siku moja TUSHIRIKI FAINALI ZA KOMBE
        HILI (msisitizo ni wa kwangu). Hili jambo linawezekana. Wapo wenzetu Afrika
        wameweza, kwa nini sisi tusiweze? Wao ni watu kama sisi, maadam wameweza na
        sisi tutaweza.
        Lakini ili tuweze hatuna budi kuiga mfano hususani waliyofanya wenzetu na
        wanayoendelea kufanya kuendeleza mpira wa miguu. Twende tukajifunze kutoka
        kwao. Lakini hata kabla ya kwenda huko, yapo mambo hatuna budi kuyafanya.
        Naomba nitaje baadhi yake:


        1. Tuimarishe Uongozi, utendaji na uendeshaji wa vilabu vya mpira. Mchezaji
        hufundishwa kucheza mpira katika Klabu yake. Hapo ndipo hufundishwa
        maarifa ya kucheza mpira na vipaji kuendelezwa. Hebu tujiulize hali ya
        vilabu vyetu vya soka ikoje. Je vinaongozwa vizuri? Vinaendeshwa vizuri?
        Jibu tunalijua sote kuwa ni hapana. Lazima suala hili tulitafakari kwa makini
        na kulipatia jawabu. Tukishindwa kupata jawabu muafaka na mambo
        yakaachwa kuendelea yalivyo, mpaka mwisho wa dunia hatutakuwa tunasogea
        popote.
        2. Tupate walimu wenye uzoefu kufundisha timu zetu. Hii ndiyo njia ya uhakika
        ya kukuza na kuendeleza vipaji na hivyo kupata wachezaji bora.
        3. Tuwekeze katika kuibua na kuendeleza vipaji vya wachezaji toka umri mdogo.
        Vilabu viwe na timu za watoto na vijana. TFF isaidie kuanzishwa kwa shule
        za mchezo wa mpira wa miguu kwa watoto na vijana. Mashuleni wapatikane
        walimu wa michezo walio wazuri kufundisha.
        4. TFF ionekane zaidi ya ilivyo sasa katika mipango ya kuendeleza soka
        mashuleni, vijijini, mitaani na vilabuni. TFF ikiwa na mipango na kuisimamia
        na kuwabana wadau kuitekeleza itasaidia. Vinginevyo TFF itabakia
        kusimamia Ligi Kuu, kutoa adhabu kwa wachezaji na kusimamia timu ya
        Taifa. Hiyo haitoshi.’’
        Mwisho wa kunukuu.
        Ndugu zangu wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF, wadau na wapenzi wa mpira wa Miguu Tanzania
        tujiulize kuanzia kipindi hicho cha 2009 hadi leo hii katika haya maagizo ya Mheshimiwa Rais Jakaya
        Mrisho Kikwete tumetekeleza yapi zaidi ya kuwa wasindikizaji katika medani ya kimataifa? Kipindi
        chote cha miaka minane iliyopita Serikali imetoa sapoti kubwa katika sekta ya mpira wa miguu kwa
        kulipia walimu wa timu za Taifa na kuhimiza makampuni kama NMB,Serengeti Breweries,Airtel,Coca
        Cola na sasa Tanzania Breweries kudhamini timu zetu za taifa na mashindano mbali mbali,matunda
        yake yako wapi? Ndo kwanza tunazidi kuporomoka kwenye viwango vya FIFA. Iweje miaka ya
        nyuma timu zetu za Taifa zilifanya vizuri wakati zinaweka kambi Salvation Army, leo zinakaa hotel za
        nyota tatu mafanikio mbona hatuyaoni? Kama TFF imeondolewa gharama za kulipa makocha, kuweka
        timu kambini, kununua vifaa vya timu, dawa, posho ,malazi pamoja na usafiri wa timu iweje leo TFF
        ishindwe kutumia vyanzo vyake vya mapato zikiwemo fedha toka FIFA na CAF kwa ajili ya
        kuanzisha na kuendeleza programmu ya vijana ya kitaifa? Kwa mujibu wa mtandao wa FIFA kati ya
        mwaka 2008 na 2012 TFF imepokea toka FIFA msaada wa jumla ya dola za kimarekani milioni moja
        na lake nane na nusu (yapata shilingi bilioni tatu za kitanzania), hizi fedha zimefanyia nini? Kwa nini
        timu za vijana hazina udhamini? Ipi timu yetu ya taifa iwe ya wanaume wakubwa (senior team) ,
        wanawake au za vijana inayoweza leo hii kujivunia mafanikio? Iko wapi ligi ya wanawake? Katika
        hili tusilaumu Chama cha mpira cha wanawake, wakiwezeshwa wanaweza.Tutapataje timu mahiri ya
        Twiga stars bila ligi ya wanawake? Katika ngazi ya klabu, hasa zinazoendeshwa kwa mfumo wa
        kijamii kama Toto Africa, Coastal Union, Yanga, Simba,Mbeya City n.k. hadi leo hii pamoja na
        rasilimali za vilabu hivi ni klabu ipi imeweza kusimamia na kujiendesha yenyewe tokana na vyanzo
        vyake yenyewe? Tuendelee kujiuliza:
        Ø Ni walimu wangapi wa mpira tumewaendeleza kufikia kiwango cha kukabidhiwa majukumu ya
        kufundisha Taifa Stars. Fursa za mafunzo tunazopewa na FIFA na CAF tunazitumiaje? Je
        tumeweza kuwa na angalau kocha mmoja anayefundisha mpira nje ya nchi kama ilivyo kwa
        akina Sam Timbe ( wa Uganda), James Sianga ( wa Kenya) Jack Chamangwana ( wa Malawi)
        na wengine ambao waliweza kufundisha mpira Tanzania kwa ufanisi?
        Ø Ni refa gani tumemuendeleza akafikia kiwango cha kuchezesha mashindano ya fainali za dunia
        au AFCON au Klabu bingwa ya Africa? Refa wa mwisho kuchezesha fainali za Mataifa Africa
        (AFCON) ni Omar Abdulkadir huko Burkina Faso mwaka 1998.
        Ø Ni program ipi ya vijana ya kuibua vipaji na kuviendeleza tuliyo nayo? Wale vijana wa Copa
        Cocacola 2007 waliopelekwa kwa mbwembwe Brazil waliishia wapi? Tuna rekodi
        zao?Tunajua wako wapi na wanafanya nini? Na hawa walioshinda majuzi Afrika Airtel Rising
        Stars tumewatangenezea program gani ya maendeleo?
        Ø Tunaelewa matatizo ya vilabu vya mpira hususani uhaba wa vifaa na pesa za uendeshaji, je
        vilabu vyetu TFF inavisaidiaje katika kuendeleza programu zao za vijana?Au kazi yetu ni kudai
        kila klabu iwe na timu ya under 20 bila kujali gharama za uendeshaji wa timu hizi?
        Ø TFF hadi sasa imebuni, kusimamia na kutekeleza program endelevu ipi ya kuendeleza soka
        mashuleni, vijijini, mitaani au vilabuni? Au mpaka tusubiri Airtel rising Star na Copa
        Cocacola? Siku wakubwa hawa wakisusa itakuwaje?
        Ø Ziko wapi juhudi za kuhimiza upatikani wa vifaa vya kufundishia mpira watoto (kama mipira
        size 3/4) pamoja na kuimarisha miradi ya kuendeleza vijana ?
        Ø Hivi timu zetu za Taifa zinatumia mfumo upi wa uchezaji? Au kila kocha wa taifa tunayemleta
        anakuja na mfumo wake? Wenzetu wameweza kubuni mifumo ya uchezaji ya timu zao za
        Taifa na wameushirikisha katika mfumo wa ufundishaji wa watoto. Lini Mwalimu wetu wa
        Taifa alikaa na walimu wa vilabu (angalau vya Premier League) ili kujadili ufundishwaji wa
        mpira nchini, hii ikiwa ni pamoja na kujadili masuala yahusuyo mbinu, lishe, huduma za afya
        na ukakamavu wa mwili? Hivi mchezaji akitoka katika klabu yake ambako amezoea kula dona
        na maharage ukampeleka kambi ya Timu ya Taifa akapewa prawns, kuku na samaki kwa siku
        nne za kambi itamsaidia kumbadili siha? Ng’ombe hanenepeshwi siku ya mnada.Uratibu wa
        programu za vilabu ni muhimu.
        Ø Raha ya mpira ni kelele na hoi hoi za mashabiki. Wataalam wa mpira wanasema umoja wa
        mashabiki wa mpira ni sawa na mchezaji wa 12 uwanjani. Zipo timu ambazo kihistoria
        zilikuwa ni za kijamii na zilihamasisha sana ligi ya Taifa, na kuiongeza hamasa na
        ushindani,Mbeya City ni mashahidi. Leo hii ziko wapi timu kama Ushirika ya Moshi, Bandari
        ya Mtwara, Kariakoo Lindi, Balimi Bukoba, Reli Kiboko ya vigogo, Kahama United, Mirambo
        ya Tabora, Tukuyu Stars, Nyota Korogwe, African Sports ya Tanga,Ujenzi Rukwa,Mji
        Mpwapwa n.k. TFF imefanya juhudi gani kufufua ushidani huu kwa kushirikiana na vyama
        vya Mikoa na Wilaya?
        Ø Wapo wachezaji wastaafu waliojitolea kwa moyo mmoja kuiletea heshima nchi yetu. Leo hii
        tunasikia kina Alfonce Modest na Jellah Mtagwa wanalalamika hawana msaada, na hao ndio
        wale waliojitolea hadharani kutoa kilio chao. TFF hadi leo hii imewahi kuandaa mpango gani
        endelevu wa kuwasaidia wachezaji wastaafu? Shirikisho la mpira barani Afrika CAF
        wameanzisha ISSA HAYATOU TRUST FUND kusaidia wachezaji wastaafu waishio katika
        mazingira magumu,sisi tumechukua hatua gani katika hili?
        Ø Iweje mpake leo hakuna mashindano yoyote ya wanawake ya kitaifa yawe ya ligi au ya
        mtoano,angalau kwa ngazi ya kanda ? TFF itawezaje kuibua vipaji vipya vya timu ya taifa ya
        wanawake TWIGA Stars bila mashindano ya aina hii?
        Ø Vilabu vya mpira, hususani vya Ligi Kuu, vimegeuka kuwa kisima cha watu kuchota fedha.
        Haiyumkiniki vilabu ambavyo vinaweka timu kambini, kuihudumai kuanzia malazi, posho,
        vifaa, madawa na usafiri mwisho wa mechi jumla ya pesa wanayopewa inakuwa chini ya nusu
        ya mapato yote ya mechi. Hayo maendeleo ya mpira ambayo yametakiwa yaanzie ngazi ya
        vilabu yatapatikanaje? Vilabu vimegeuka vitega uchumi vya watu wengine wakati vyenyewe
        vinataabika na kujiendesha kwa mateso makubwa.
        Ya kusema ni mengi, kwa leo tuishie hapa.

        Nini matokeo ya hali hii? Takwimu hazidanganyi. Matokeo ya hali hii ni timu za Taifa kushuka
        viwango katika orodha ya FIFA siku hadi siku. Viwango vya timu za taifa vinapimwa kwa kuangalia
        uwiano wa matokeo ya timu ya wakubwa (senior) pamoja na yale ya timu nyingine za vijana za nchi
        husika. Miaka ya mwanzo ya tisini tulishawahi kupanda hadi nafasi ya 65, leo hii kila kukicha tuko
        kwenye 120.Kuporomoka huku kutaendelea hadi lini?
        Ndugu zangu, tujiulize wapi tumetoka, tuko wapi na tunataka kuelekea wapi? Jibu ni rahisi, kama
        alivyoagiza Mh Rais Kikwete,tujipange upya, tubuni mkakati wa uendelezaji wa mpira, tuandae
        program endelevu yenye malengo yanayopimika na kwa pamoja tukishirikiana na Serikali, FIFA
        CAF na CECAFA,Halmashauri, Taasisi zisizo za kiserikali, Sekta binafsi, Vyombo vya habari na
        wadau wengine wote wa mpira wa miguu tutaweza kufanya vizuri na kuifanya Tanzania isifike
        duniani kote. Katika kutimiza azma hii sharti tuanzie kwa kuleta mabadiliko ya uongozi wa juu wa
        TFF, tupate kiongozi ambaye sio sehemu ya mapungufu ya TFF,hakuna njia ya mkato.Mimi Jamal
        Emil Malinzi,nimejipima na ninaamini nina uwezo wa kutosha wa kubuni, kuratibu na
        kusimamia mabadiliko haya nikiwa Rais wa TFF.
        Ndugu zangu, siku zote si vyema kukosoa bila kueleza njia mbadala ya kufuata ili kutatua tatizo. Hapa
        tunazungumzia mpira wa miguu na namna ya kuunasua toka kwenye janga la kushuka kiwango na
        timu zetu za Taifa kuendelea kugeuzwa kichwa cha mwenda wazimu ambacho hadi majuzi vibonde
        Gambia wamejifunzia kunyoa.
        Ili tuweze kuukwamua mpira wetu ni vyema tukakumbushana kuwa ili mpira uendelee unahitaji vitu
        vinne:
        1. Vipaji;
        2. Walimu;
        3. Vifaa;
        4. Viwanja
        1. Vipaji
        Tanzania ni nchi yenye watu zaidi ya milioni 44. Nchi ya Cape Verde yenye watu 500,000 tu
        imeweza pamoja na uchache wake kuvumbua vijana 11 ambao wameweza kuifikisha nchi yao
        fainali za Africa 2013 Afrika Kusini na majuzi nusura waende kombe la dunia kama sio tatizo
        la utunzaji kumbukumbu. Sayansi ya uibuaji vipaji (scouting) ni muhimu na si kila mtu
        anaijua. Watafutwe wanaoijua, watufanyie kazi ya kutuibulia vipaji vipya, na katika hili ni
        sharti mpira wa ushindani uchezwe nchini kote ili vipaji vionekane.
        2. Walimu
        Mpira ni sayansi,mpira ni taaluma. Kipaji bila mwalimu wa kukiendeleza ni bure. Vijana
        mpira wanaanza kuucheza wakiwa wadogo hususani wakiwa shule za msingi. Huko ndiko
        Taifa linahitaji kusambaza walimu wenye taaluma ya kufundisha mpira ngazi ya awali.
        Wakishakuzwa kimpira ni lazima wawepo walimu wa kutosha kuwaendeleza ngazi ya
        wakubwa na Taifa. Leo hii Uingereza ina walimu 1100 wenye leseni daraja A,Ujerumani wapo
        5500 na Hispania 12,000,Tanzania tunaye mmoja tu,kwa mtaji huu tutafika kweli?Kwa mujibu
        wa ripoti ya TFF nchi nzima ya Tanzania ina walimu wa mpira wa madaraja yote elfu mbili tu
        na mia tano kati yao wako Dar es salaam. Hawa walimu 2000 ndio wanategemewa
        wawafundishe mpira vijana wa Kitanzania zaidi ya milioni kumi walio katika umri wa
        kufundishwa mpira!
        3. Vifaa
        Wachezaji, walimu wa mpira, madaktari na waamuzi wote wanahitaji vifaa vya msingi ili
        mpira uchezwe. Nchini mwetu vijana walio wengi wanacheza pekupeku, jezi ni upande mmoja
        kucheza kifua wazi, mpira ni wa kuviringisha matambara, refa anavaa suruali, filimbi ni mluzi,
        magoli hayana nyavu, n.k. Hii ndiyo hali halisi ya uchezwaji wa mpira maeneo mengi
        Tanzania hasa vijijini ambako ndiko kunapaswa kuwa chimbuko kubwa la vipaji.
        Gharama za vifaa vya michezo ziko juu mno, mfano mpira mzuri unaofaa kuchezewa kwenye
        ardhi ngumu (rough surface) bei yake ni shilingi laki tatu, shule ipi ya msingi itaweza
        kuununua huu mpira? Kuna baadhi ya vyombo vya habari majuzi viliripoti kuwa kuna
        mchezaji alifunga hat trick ngazi ya Ligi Taifa akanyimwa mpira kisa ni wa thamani kubwa.
        Mamlaka husika, hasa za kodi zinapaswa kuliangalia hili, ili upatikane unafuu katika bei za
        vifaa vya michezo maana karibia vyote vinaagizwa toka nje. Lakini pia vifaa vya michezo vya
        misaada vinavyopatikana kutokana na miradi mbalimbali ya TFF ni juu ya TFF kuhakikisha
        vinafikishwa vijijini pia kupitia vyama vya mikoa na wilaya.
        4. Viwanja
        Wilayani Ngara mkoani Kagera kuna uwanja wa mpira unaitwa ‘’Uwanja wa Changarawe’’ na ni
        kweli uwanja huo umejaa changarawe. Beki akikaba kwa mtindo wa kuteleza ardhini ‘sliding tackle’
        basi nyama ya paja anaiacha pale chini. Hii ndiyo hali halisi ya viwanja vyetu vingi nchini, kama vipo
        ni vibovu sana maana maeneo mengi viwanja vya mpira hakuna vimechukuliwa na wajanja wachache
        na kugeuzwa makazi na majengo ya biashara. Tunahitaji viwanja vyenye ubora ili vijana wetu
        wafundishwe mpira wa kisasa kwa ufanisi, mpira wa kupiga pasi ya chini. TFF kwa kushirikiana na
        vyama vya Mikoa na Wilaya sharti wawe mstari wa mbele katika kulipigania hili.
        AHADI YANGU
        Endapo nitachaguliwa kuwa Rais wa TFF, kwa kushirikiana na viongozi wote wa TFF kuanzia ngazi
        ya vilabu, Wilaya, Mikoa na Kamati ya Utendaji Taifa na kwa kuhusisha kwa karibu Vyama vya
        kimataifa vya FIFA na CAF, Serikali, Halmashauri,Taasisi zisizo za kiserikali, Vyombo vya habari,
        Sekta binafsi, Mashirika ya umma na wadau wa mpira wa miguu Tanzania ninaahidi kuenzi mafanikio
        ya awamu inayomaliza muda wake , kustawisha utulivu katika uendeshaji wa mpira, na kufanya
        jitihada za kubuni, kuboresha na kustawisha maendeleo ya mpira wa miguu Tanzania. Jitihada kubwa
        zitawekwa kwenye maeneo makuu yafuatayo:
        1. Ufundi (Technical)
        1.1 Muundo wa Idara ya Ufundi
        Katiba ya TFF imeainisha wazi kuwa TFF ndiye msimamizi mkuu wa mpira wa miguu
        Tanzania, hivyo jukumu la kuleta maendeleo ya mchezo huu kwa kiasi kikubwa linaiangukia
        TFF.Ni kwa msingi huu basi asilimia kubwa ya rasilimali za TFF lazima iwekezwe katika
        kuleta maendeleo ya mpira. Kwa mfumo wetu wa uendeshaji, kichocheo kikuu cha maendeleo
        ya mpira ni idara ya ufundi ya TFF. Hivyo idara hii ya ufundi inapaswa kuwa ndiyo idara
        mama ya TFF ambayo inapaswa kuongoza kwa matumizi ya fedha, idadi ya waajiriwa na
        matumizi ya rasilimali nyingine za TFF . Kwa sasa pale TFF hali sivyo ilivyo. Iwapo
        nitachaguliwa nitapendekeza jukumu la kwanza la Kamati ya utendaji liwe ni kurekebisha na
        kuboresha mfumo wa uendeshaji wa idara ya ufundi. Nitapendekeza idara ya ufundi iendelee
        kuongozwa na Mkurugenzi wa Ufundi na chini yake awe na wakurugenzi wasaidizi wa vitengo
        watatu Mkurugenzi Msaidizi (ufundi), Mkurugenzi Msaidizi (Elimu na Mafunzo) ambaye kwa
        sasa anaitwa Education officer, na Mkurugenzi Msaidizi (Maendeleo ya mpira).
        Kitengo cha Ufundi kitahusika na kubuni na kusimamia shughuli zote zinazohusu maendeleo
        ya Timu za Taifa kuanzia za wakubwa hadi za vijana. Hii itakuwa ni pamoja na kuandaa
        mitaala ya taifa (national football curriculum) ya ufundishaji wa mpira Tanzania kuanzia umri
        wa miaka mitano hadi watu wazima. Walimu wa Timu za Taifa wataripoti kwake.
        Kitengo cha Elimu na Mafunzo kitahusika na kubuni na kuratibu kozi zote na mafunzo yote
        yanayohusiana na mpira kama vile kozi za Marefa, Makocha, Madaktari, Makamisaa,
        Watawala, Waandishi wa Habari za Michezo, n.k.
        Kitengo cha Maendeleo ya mpira kitahusika na kubuni,kuratibu na kusimamia mpango wa
        maendeleo ya vijana (grassroot) na kutafuta vipaji (scouting). Kitengo hiki kitafanya kazi kwa
        kushirikiana kwa ukaribu na idara za Serikali hasa idara za Elimu,Vijana na TAMISEMI,
        Halmashauri,Mashirika ya umma,Sekta binafsi pamoja na Taasisi nyingine za kijamii.
        Wakuu wa vitengo hivi wataajiriwa kwa kufuata vigezo makini na bila upendeleo wala
        kujuana.
        1.2 Ujenzi wa Kituo cha Mpira (Football Centre of excellency)
        Hiki ni Kituo Maalum cha mafunzo ya mpira wa miguu. Katika kituo hiki kunakuwa na kila
        aina ya miundo mbinu, viwanja vya kufundishia mpira, vituo vya tiba,madarasa ,maabara za
        utafiti,hosteli n.k Kituo hiki pia kinakuwa ndio sehemu kuu ya kuweka kambi za timu za Taifa
        na kutoa mafunzo ya ufundi yakiwemo ya ukocha, urefa, utawala na tiba. Wenzetu wa Senegal
        na Ethiopia kwa kushirikiana na Shirikisho la Mpira Africa CAF wameweza kujenga vituo hivi
        na matokeo yake tunayaona.Cameroon pia wana kituo hiki.
        Pamoja na gharama zake kuwa kubwa, cha muhimu hapa ni kuweka nia, kutafuta ardhi kwa
        kushirikiana na Serikali na kuanza ujenzi taratibu.Kwa kuwa klabu ya Sunderland ya Uingereza
        na kampuni ya kufua umeme ya Symbion wameonyesha nia ya kushirikiana naSerikali kujenga
        kituo cha michezo itakuwa vyema iwapo TFF itashirikiana na taasisi hizi muhimu ili kufikia
        azma ya kujenga kituo hiki cha kisasa. Iwapo nitachaguliwa nitasimamia uanzishwaji wa mradi
        huu muhimu ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kulikomboa soka letu.
        Aidha uwanja wa Karume yalipo makao makuu ya TFF utazungushiwa jukwaa ili mechi
        ambazo sio kubwa zifanyike pale, Hii itaiongezea TFF mapato na vilabu pia.
        1.3 Timu Kupanda Daraja
        Ili kuongeza ushindani na kupanua mpira uchezwe kona zote za nchini ( to spread the game)
        ,mtindo wa kucheza kikanda ili kupata timu za kupanda daraja kuu utakuwa ni wa kudumu na
        utaimarishwa kwa kutafutiwa udhamini na kuboreshwa viwanja kwa kushirikiana na wamiliki
        wa viwanja hivyo. Usimamizi wa mashindano ngazi hii utaimarishwa na kusimamiwa kwa
        karibu zaidi ili timu itakayopanda daraja iwe imepanda kwa haki na hivyo kuleta ushindani
        Ligi Kuu.
        Hata hivyo waraka uliotolewa na TFF ukiagiza mikoa ichezeshe ligi ili kupata bingwa wa
        mkoa utafutwa kwa sababu hautekelezeki kutokana na hali ya uchumi na uhalisia wa jiografia
        ya mikoa ya Tanzania. Mathalani Mkoa wa Mtwara ukichezesha ligi ya mkoa (kwa maana ya
        nyumbani na ugenini) ina maana bingwa wa Wilaya ya Masasi atasafiri vipi akacheze
        Newala au Mkoani Lindi bingwa wa Liwale atasafiri vipi akacheze na bingwa wa Kilwa ,
        Pwani bingwa wa Mafia atasafiri kwa gharama za nani akacheze Bagamoyo na wa Kibaha
        akacheze Utete? Pamoja na nia njema ya TFF uhalisia hauruhusu. Kama Mwenyekiti wa chama
        cha mpira mkoa wa Kagera nalijua hili, hakuna haja ya TFF kuwa inatoa maelekezo ambayo
        hayatekelezeki, hasa ukizingatia kuwa TFF hakuna msaada wanaopeleka kusaidia mikoa na
        wilaya ziandae mashindano yao.Vyama vya mikoa na wilaya viachwe viendelee kutumia
        ubunifu wao kupata mabingwa wao kulingana na hali halisi ya mazingira yao.
        1.4 Kuanzisha mashindano mapya na kufufua ya zamani
        Wataalam wa kandanda wanasema kuwa ili mchezaji awe katika kiwango bora inabidi acheze
        kwa mwaka kimashindano wastani wa mechi 40. Ligi yetu kuu,Vodacom premier
        league,inatoa fursa kwa mchezaji kucheza michezo 26 kwa mwaka iwapo anapangwa kila
        mechi.Hii haitoshi. Namna pekee ya kurekebisha hali hii ni kuongeza idadi ya mashindano kwa
        mwaka.Hili litafanyika kwa kufufua kombe la Taifa (Taifa cup) na kuanzisha kombe la
        shirikisho (kama FA cup ya Uingereza). Kombe la shirikisho litashirikisha timu zote nchini
        kuanzia ngazi ya kata,tarafa,wilaya,mkoa hadi Taifa na bingwa wake atawakilisha nchi katika
        kombe la shirikisho la Afrika CAF confederation cup (kama ilivyo Kenya kwa sasa).
        1.5. Mpira wa Wanawake
        Hadi sasa hatuna mfumo imara na unaoeleweka wa kuendeleza soka la kinamama. Mpira wa
        wanawake umeanzia Wilaya ya Kinondoni, ukakulia Wilaya ya Kinondoni na umegotea
        Wilaya ya Kinondoni ambako kuna timu zenye majina kama Mburahati Queens na Sayari
        Queens. Mpira wa wanawake sharti usambae nchi nzima, na ili kufanikisha azma hii lazima
        yaanzishwe mashindano ya kitaifa ya wanawake ikiwemo Ligi ya taifa ya wanawake. Hii
        itaendana na juhudi za kuongeza makocha, waamuzi na makamisaa wanawake na kutafuta
        udhamini kwa timu ya Taifa ya wanawake TWIGA STARS.
        1.6 Maandalizi ya Vijana (Grassroot Programme)
        Mpango endelevu wa maendeleo ya soka la vijana sharti uandaliwe, uratibiwe na kusimamiwa
        kwa makini. Program madhubuti ya maendeleo ya mpira wa vijana lazima ibuniwe ,iratibiwe
        na kusimamiwa kwa usatadi mkubwa.Mradi huu lazima ulenge ,kwa hatua,kufikia hatua ya
        kuingiza timu zetu fainali za kombe la Afrika la vijana chini ya umri wa miaka 17 na 20,fainali
        za olimpiki, fainali za Afrika wachezaji wa ndani CHAN,fainali za Afrika AFCON na mwisho
        fainali za kombe la dunia.Hii itakuwa ni pamoja na kujiwekea utaratibu wa mzuri wa
        kuhakikisha vijana wetu wanapata fursa ya kucheza mpira nje ya nchi ili kujiongezea
        umahiri.Na hii ni kwa wanawake na wanaume.
        Mpango huu ni lazima ushirikishe Serikali Kuu (hasa Wizara zenye dhamana ya Michezo,
        Elimu na Halmashauri), Taasisi zisizo za kiserikali,mashirika ya umma,sekta binafsi na
        TFF,CAF na FIFA. Ushirikishwaji wa Serikali na Halmashauri katika program hii ni muhimu
        sana kwa kuwa ndio wasimamizi na wamiliki wa shule nyingi za msingi ambako ndiko vijana
        wetu wanakoanzia kucheza mpira. Mpango kazi huu lazima uonyeshe:
        1. Nini tunataka kufanikisha.
        2. Utaratibu utakaotumika.
        3. Nguvu kazi inayotakiwa na sifa zake.
        4. Mwongozo wa kufuatilia kupima ufanisi wa programu.
        5. Kupambanua gharama za mpango na taratibu za uchangiaji wake.
        Hatua muhimu katika kufanikisha program hii zitakuwa ni:
        -Kufundisha walimu wa walimu (instructors), hawa ndio watakuwa chachu ya kupata
        walimu wa mpira mashuleni na mitaani.
        -Walimu wa walimu (instructors) kufundisha walimu wa kutosha wa michezo mashuleni na
        mitaani
        -Kwa kushirikiana na wamiliki wa shule kuhakikisha viwanja vya kuchezea vinakidhi
        viwango
        -Kutafuta na kusambaza vifaa vya michezo mashuleni hasa mipira ya saizi muafaka kwa
        mujibu wa viwango vya kimataifa.
        -Kupata shule angalau moja kila mkoa itakayopokea watoto wenye vipaji maalum vya
        kucheza mpira, pale ambapo wazazi hawataweza kuwalipia karo vijana hawa basi TFF
        ihakikishe karo zao zinapatikana,huo ndio uwekezaji katika mpira.
        -Kuandaa mashindano mbali mbali yatakayoshirikisha shule hizi ili kupata timu za taifa za
        vijana wa umri mdogo wa kike na wa kiume.
        -Kuhakikisha timu hizi za umri mdogo zinapata fursa ya kushiriki mashindano mbali mbali
        ya kimataifa
        - Kupata vikosi vizuri vya timu za taifa za vijana wa umri mdogo ambao watakua pamoja,
        hao ndio watajenga msingi imara wa timu za Taifa za wakubwa kwa miaka ya baadae.
        Itakuwa ni muhimu sana program hii iendane vizuri na ratiba nyingine za mashindano ya
        kitaifa kama Umitashumta, Umisseta, Airtel rising star, Copa Coca Cola n.k.
        - Kuanzisha mashindano ya kitaifa ya kombaini za shule za sekondari na ya kombaini za
        vyuo vikuu. Wachezaji mahiri wa timu ya taifa kama Leodeger Chilla Tenga (Rais wa
        TFF) na Leopold Tasso Mkebezi (meneja wa Taifa stars) waliibukia kwenye
        mashindano kama haya Mkebezi akiwa beki wa kombaini ya sekondari za
        Bukoba,Ihungo,Kahororo na Nyakato.
        Aidha vituo vya michezo (sports academies) ambavyo tayari vipo vitatengenezewa utaratibu
        wa usajili na kuwekewa utaribu wa kuviendesha.
        Ili kuondoa ulalamishi wa vituo vya mafunzo (Academies) kulalamikia malipo pindi mchezaji
        akisajiliwa timu kubwa, vituo vyote vya vijana vitasajiliwa na vijana wao wote wataingizwa
        kwenye kumbukumbu za TFF (data base) kwa majina, saini na picha,hii itasaidia kuzuia sakata
        kama la Mbwana Samata na klabu yake ya utotoni ya Mbagala maana kumbukumbu za TFF
        zitakuwa ndio jibu la maswali yote.
        1.7 Tiba
        1. Tutaimarisha usalama uwanjani. Tutahimiza kila uwanja zinakochezwa mechi za ligi kuwe na
        gari la wagonjwa na chumba cha dharura (emergency room).
        Katika kuimarisha usalama tutahakikisha vifaa muhimu vya dharura kama vifaa vya hewa
        (oxygen) na vifaa vya kushtua moyo (defibulator) vinakuwepo. Kwa sasa hapa Tanzania
        uwanja pekee wenye vifaa hivi ni Uwanja wa Azam Chamazi. Ni jambo la kusikitisha kuona
        hata uwanja mpya wa Taifa hauna chumba cha tiba dharura (emergency room) na kibaya zaidi
        makato ya uwanja hayaendi kuanzisha huduma hii muhimu wakati viongozi mbalimbali wa
        kitaifa wanahudhuria mechi uwanjani.
        2. Mradi wa Goal Project wa FIFA unatoa pesa za tiba na mradi huu uliweka lengo la kuwa na
        chumba cha kliniki pale uwanja wa Karume. Tutakifufua chumba hiki, tutakiwekea vifaa na
        kuhakikisha huduma ya kliniki kwa wanamichezo iliyokuwa ikitolewa na madaktari kila
        Jumapili inarudishwa. Posho itatafutwa ili madaktari watoa huduma angalau wapate nauli na
        maji ya kunywa.
        3. Wakati wa kujadiliana mikataba na wadhamini mbalimbali tutahakikisha kipengele cha
        huduma za afya kinaingizwa katika mikataba. Udhamini utatafutwa kwa ajili ya vipimo vya
        wachezaji kabla ya league (pre-league medical test) kama vile vipimo vya uvumilivu (Yo-Yo
        test) na vipimo vya moyo (cardiac tests). Hii ni kwa ajili ya usalama wa wachezaji na
        waamuzi.
        4. Hadi leo chama cha Madaktari Tanzania, TASMA hakina ofisi. Hii ni aibu kwa chama chenye
        hadhi na umuhimu wa kipekee kama hiki. Tutahakikisha TASMA inapata ofisi yake pamoja
        na chumba maalum cha kliniki.
        5. Huduma ya afya lazima iwe sehemu maalum ya mfumo wa idara ya ufundi. Ni muhimu timu
        ya madaktari wa Timu ya Taifa (National Medical team) ijulikane ni kina nani na wapewe
        mikataba ya kazi. Hii tutalipigania.
        6. Majeraha ya michezo huwa yanahitaji utaalam wake wa tiba. Tutaiomba Serikali itupe
        ushirikiano ili kipatikane kitengo maalum cha kutibu majeraha ya wanamichezo (sports
        injuries wing) katika baadhi ya hospitali zetu wakati tunajiandaa kuwa na kitengo cha tiba
        (Rehabilitation Centre) katika kituo cha michezo kitakachojengwa.
        7. Ili kuimarisha uwezo wa madaktari wetu kutoa huduma za afya kwa wanamichezo,
        tutahakikisha madaktari wengi kadiri iwezekanavyo wanapata kozi za msingi,kati na juu
        (preliminary,intermediate and advanced). Nafasi hizi zitatolewa bila upendeleo wala kujuana.
        8. Utoaji wa ushauri nasaha kwa wachezaji utaongezeka hasa kuhusu masuala ya ukimwi na
        madhara ya madawa ya kuongeza nguvu na ya kulevya.
        1.8 Waamuzi
        Imepita miaka zaidi ya 15 toka Tanzania itoe mwamuzi wa kimataifa wa kuchezesha fainali kubwa
        (mara ya mwisho AFCON 1998), hii si sawa. Utaratibu uliopo sasa wa kuwapata na kuwaendeleza
        waamuzi ama una mapungufu au haufai kabisa hivyo budi utafutwe utaratibu ulio mzuri zaidi katika
        kupata waamuzi bora, tafiti zitafanywa ili kubaini ni njia zipi za kisayansi za kuwapata waamuzi bora
        (Top referees).Semina za mara kwa mara za CAF na FIFA ni nzuri lakini hazitoshi, TFF lazima
        iwekeze kwa kutoa mafunzo zaidi ya waamuzi kwa gharama zake.
        Aidha mradi wa maendeleo ya mpira kwa vijana (grassroot) utahusisha pia mafunzo ya uamuzi wa
        mpira kwa vijana kama kinavyofanya kituo cha Jenerali Twalipo.
        Utaratibu wa kutoa adhabu kwa waamuzi wanaosemekana wameboronga uwanjani nao unahitaji
        marekebisho ya haraka sana. Uamuzi wa mpira ni taaluma kama zilivyo taaluma nyingine,mwamuzi
        akikosea ni vyema akakosolewa na mwamuzi mwenzie ambaye ni mwandamizi,na kama ni
        kuadhibiwa aadhibiwe na jopo la waamuzi wenzie waandamizi lakini wastaafu na sio mtu mwingine
        ambaye hajawahi kupuliza filimbi.
        1.9 Makocha
        Kumekuweko na utamaduni usiofaa katika soka la Tanzania miaka ya karibuni wa kuona kuwa
        makocha wa kigeni ndio bora zaidi na wanastahili mikataba, mishahara minono na marupurupu
        ilhali makocha wazawa wanageuzwa ‘deiwaka’, jambo hili ni baya sana, ajira ziheshimiwe kwa
        msingi wa taaluma na sio kwa msingi wa nchi atokayo mtu.
        Makocha wetu wazalendo wana uwezo mkubwa kama wakipewa nyenzo kama wanazopatiwa
        wageni, kama malipo mazuri, mikataba ya muda mrefu, vitendea kazi na kuheshimiwa program
        zao bila kuingiliwa na viongozi.Iwapo nitachaguliwa ninaahidi:
        - Kuwaendeleza makocha kimafunzo ndani na nje ya nchi kwa wale wenye uwezo na
        utashi wa kufanya hivyo.
        - Kushawishi taasisi za elimu nchini kama vyuo vikuu kufundisha taaluma ya ukocha
        - Kuhakikisha walimu wa mpira wa timu zetu za Taifa wanakuwa na mikataba stahiki, hii
        ni pamoja na benchi zima la ufundi.
        - Kuwajengea uwezo makocha wetu wazalendo ili nao wapate fursa ya kufundisha mpira
        nje ya nchi.
        - Kuanzisha tuzo za kila mwaka za makocha wazalendo ambao wamefanya vizuri katika
        ufundishaji wa soka la vijana la wanawake na wanaume.
        - Kuhakikisha utaratibu wa leseni za CAF unazingatia vigezo vya kitaaluma, uzoefu na
        ushiriki wa kocha mhusika katika ufundishaji. Makocha ambao wanafundisha (active
        coaches) watapewa kipaumbele katika kupata kozi za kupanda madaraja kuliko wale
        wanaofungia vyeti makabatini.Leseni za CAF ni muhimu katika kumfanya mwalimu wa
        mpira atambulike kimataifa.
        - Kuhakikisha kanuni za ligi zinasimamiwa vyema ikiwemo kanuni itakayomlazimisha
        kila mwalimu wa ligi kuu na daraja la kwanza awe mwanachama wa TAFCA (chama
        cha makocha nchini), walimu wa kigeni watapewa uanachama wa muda.
        1.10 Timu za Taifa
        Timu zetu za Taifa, ziwe za wakubwa au za vijana ndio kioo cha mpira wa Tanzania. Jitihada
        zote lazima zifanyike kuhakikisha tunakuwa na timu nzuri za Taifa kuanzia za wakubwa
        (wanawake/wanaume) hadi za vijana. Pamoja na jitihada zitakazofanyika kuboresha idara ya
        ufundi kama ilivyoanishwa hapo juu lakini pia yafuatayo ni mambo ya ziada yatakayofanyika.
        (a) Kuandaa fainali za Afrika za umri chini ya miaka 17 (U-17) mwaka 2019
        Hadi sasa hakuna nchi ambayo imekwisha pata uenyeji wa mashindano haya. Uenyeji huu
        unatolewa na Shirikisho la vyama vya mpira Afrika CAF.Hii ni changamoto kwetu
        Watanzania kuomba uenyeji huu.Tukipewa fursa hii itatusaidia sana kutusukuma tuanze
        kuandaa programu ya nguvu ya miaka mitano ya kupata timu yetu itakayocheza katika
        fainali hizi kama wenyeji. Aidha kama nchi tutalazimika kuboresha miundo mbinu yetu
        hususani viwanja vyetu vya mpira, jambo ambalo litatusaidia siku za usoni. Ninaamini
        uwezo wa kuandaa mashindano haya kama nchi tunao. Nikichaguliwa nitalisimamia hili.
        (b) Nidhamu
        TFF itaandaa Kanuni za Nidhamu (code of ethics) kwa wachezaji, walimu na viongozi wa
        Timu za Taifa mara wawapo ndani na nje ya uwanja. Hii itasaidia kujenga nidhamu ya
        timu. Kanuni hizi zitaendana sambamba na kanuni za maadili za TFF.
        (c) Walimu
        Ni vyema siku za usoni timu zetu zote za Taifa zikafundishwa na makocha wazawa.
        Utaratibu utafanyika kuhakikisha makocha wasaidizi ambao ni wazawa wanaendelezwa
        kufikia kiwango hicho, hii itakuwa ni pamoja na kuwapatia fursa za mafunzo ndani na nje
        ya nchi.
        (d) Zanzibar
        TFF kwa kushirikiana na Chama cha Mpira Zanzibar ZFA tutahakikisha kunakuwa na
        mahusiano ya karibu ya walimu wa timu za Taifa Zanzibar na Bara ili kuhakikisha timu
        bora ya Taifa inaundwa na vijana wa pande mbili za Muungano. Aidha jitahada za Zanzibar
        kuwa mwanachama kamili wa CAF na FIFA zitaendelea kuungwa mkono.
        2. Utawala
        Inabidi tuendeleze utamaduni wa kuendesha shughuli za TFF kitaasisi (to have a corporate
        culture).Nguzo muhimu za uendeshaji shirikisho kitaaluma ni pamoja na kujenga nidhamu ya
        wafanyakazi,heshima kwa uongozi,utunzaji wa kumbukumbu,ukarimu kwa wageni,umakini
        katika manunuzi na utunzaji wa fedha pamoja na kufanya kazi kwa malengo na kuhakikisha
        malengo hayo yamefikiwa.
        Maeneo yafuatayo yataboreshwa ili kuongeza ufanisi:
        2.1 Ofisi za Mikoa na Vyama Shiriki
        Kwa kuzingatia vyama vya Mikoa kuwa ndio muendelezo mkuu wa shughuli za TFF Mikoani,
        ni muhimu ofisi za mikoa zikawa kielelezo cha ufanisi wa utendaji wa TFF. Ofisi za Mikoa
        zitaboreshwa hasa kwa kupewa vitendea kazi hususani vifaa vya mawasiliano.
        Vyama shiriki hadi sasa havina ofisi zenye hadhi ya vyama hivi, tutahakikisha tunaondoa aibu
        hii. Aidha kutokana na mapato ya TFF sehemu ya mapato haya itatengwa kwa ajili ya ruzuku
        ya kupeleka kwenye vyama vya Mikoa na vyama shiriki ili isaidie kupunguza makali ya
        kuendesha vyama vyetu.
        2.2 Ofisi ya Rais
        Kutakuwa na ofisi ya Rais wa TFF. Ofisi ya Rais wa TFF (office of the President) lazima
        iimarishwe na iwe sehemu itakayoweza kukabiliana na changamoto za maendeleo ya mpira
        wa miguu. Rais wa TFF ndiye msimamizi mkuu wa shughuli za mpira wa nchi hii,lazima
        awe na mahali stahili pa kufanyia kazi kulingana na hadhi yake.Hii itakuwa ni pamoja na
        kuwa na wasaidizi wenye uweledi wa kutosha katika shughuli za kila siku za kuongoza
        shirikisho.
        Ofisi za TFF makao makuu uwanja wa Karume zitakarabatiwa na kuongeza nafasi ya
        kufanyia kazi.
        2.3 Maslahi
        Maslahi ya wafanyakazi wa TFF yataboreshwa ili kuwaongezea motisha. Hii itakuwa ni
        pamoja na kuwapa fursa ya kuhudhuria mafunzo mbalimbali.
        2.4 Vilabu vya Mpira
        Vilabu vitasaidiwa kupewa mwongozo wa kujiendesha kwa ufanisi zaidi. Aidha utaratibu wa
        mgawanyo wa mapato ya milangoni utatazamwa upya kwa lengo la kuhakikisha vilabu
        vinapata mgao mkubwa kuliko iliyo sasa. Hii ni kwa kuzingatia gharama kubwa wanazoingia
        vilabu katika kuandaa timu ikiwemo malazi, usafiri, vifaa, posho, dawa, mishahara n.k.
        2.5 Wachezaji wastaafu
        Hii ni hazina ya Taifa,kustaafu kwao kucheza mpira sio mwisho wao wa kuchangia maendeleo
        ya mpira wa nchi yetu.Jitihada zitafanyika kuanzisha mfuko maalum (Trust Fund) ambao
        utachangiwa na wachezaji wenyewe wanapokuwa bado dimbani pamoja na TFF, hii ni kwa ajili
        ya kuwasaidia hapo baadae wanapokuwa na matatizo hasa ya ugonjwa. Aidha chama cha
        wachezaji wastaafu (SPUTANZA) kitapewa ofisi na kitaimarishwa ili kiwe kiungo muhimu
        kati ya wachezaji na TFF.Wachezaji watahimizwa watumie chama hiki kutatua matatizo yao na
        chama kitapewa fursa kikanuni ya kuwa mtetezi mkuu na msimamizi wa maslahi ya wachezaji.
        2.6 Mikataba
        Utaratibu wa TFF kuingia mikataba na wadhamini mbalimbali utarekebishwa ili kuongeza
        uwazi. Ipo mikataba ambayo imesainiwa na TFF ambayo imesababisha vyama vya mikoa na
        wilaya, pamoja na uhaba wao wa pesa, wahangaike kutafuta fedha za zaida kuandaa timu zao
        kwa ajili ya mashindano yanayobeba jina la mdhamini kwa kuwa fedha anayotoa mdhamini
        haikidhi uendeshaji wa mashindano yenyewe.
        Aidha vipengele tata vinavyokandamiza maslahi ya vilabu katika baadhi ya mikataba
        inayosainiwa kati ya TFF na wadhamini vitarekebishwa kama sio kuondolewa kabisa kwa
        maslahi ya ustawi wa mpira wetu. Haki za vilabu katika matangazo ya biashara yahusuyo
        mpira zitalindwa kwa nguvu zote.
        2.7 Utaratibu wa Mashindano
        Yapo mashindano ya vijana kama Umiseta na Umitashumta yanayoandaliwa na Serikali. Kuna
        wakati mashindano kama haya yanafanyika sambamba na mashindano yanayoandaliwa na TFF
        kama vile Copa Coca Cola. Yote haya ni mashindano ya vijana, na washiriki wanakuwa ni
        vijana toka shule hizo hizo. Kwa nini tugombee fito wakati tunajenga nyumba moja? Ni
        vyema kalenda ya mashindano ya vijana kitaifa ikaandaliwa kwa pamoja kati ya Serikali na
        TFF.
        2.8 Usajili wa Vyama vya Mpira vya Wanawake
        Usajili huu haujakamilika nchini nzima hususani ngazi ya wilaya. Juhudi zitafanyika
        kukamilisha zoezi hili ili mpira wa wanawake uenee kote Tanzania.
        2.9 Kitengo cha habari
        Kitengo hiki kitaboreshwa kwa kuongezewa nyenzo za kufanyia kazi na kukipatia fursa zaidi
        za mafunzo. Aidha majukumu yake yataongezwa ili pia kishughulikie mahusiano ya
        kimataifa.Hivyo kama nikichaguliwa nitapendekeza mkuu wake aitwe ‘Afisa habari na
        mahusiano ya kimataifa’.
        3. Masoko na Uwekezaji
        Mpira unaendeshwa kwa fedha nyingi. TFF ili iweze kujiendesha kwa ufanisi ni lazima iwe na
        vyanzo vya uhakikika vya mapato. Ili kufanikisha azma hii kitengo cha masoko na uwekezaji
        kitahakikisha kwamba:
        1. TFF inatengeneza utaratibu mzuri wa kuuza bidhaa zake ndani na nje ya nchi kwa kupitia
        uuzaji wa kawaida na wa mtandao.Mikataba itaandaliwa ili kudhibiti uuzwaji holela wa
        bidhaa za TFF.
        2. Vyumba vya Maduka vinajengwa kuzunguka uwanja wa Karume na kukodishwa.
        3. Jengo la kitega cha uchumi litajengwa kwenye ardhi ya Uwanja wa Karume.Pia jukwaa la
        watazamaji litajengwa uwanja wa Karume ili mechi ambazo sio kubwa ziweze kufanyika
        pale, hii itaviongezea vilabu mapato.
        4. Juhudi za kuboresha ukusanyaji, usimamizi na mgawanyo wa haki wa mapato ya milangoni
        yatokanayo na ligi yetu utaboreshwa ikiwa ni pamoja na kubuni vyanzo vipya kupitia njia
        mbali mbali zikiwemo za udhamini mbadala kwa vilabu.Aidha jitihada ambazo tayari
        zimekwisha anza za kuunda bodi ya kuendesha ligi na uanzishwaji wa utaratibu huru wa
        kuendesha ligi zitaendelezwa ili kuongeza ufanisi,kuinua mapato ya vilabu na kuongeza
        msisimko wa ligi.Ninaunga mkono juhudi hizi.
        5. Viwanja vingi vya mpira nchini vinamilikiwa aidha na Halmashauri,Serikali kuu
        au vyama vya siasa.Viwanja hivi vingi viko katika hali mbaya kuanzia nyasi ,hali
        ya uzio,vyumba vya kubadilishia nguo,mageti,vifaa vya kuzimia moto n.k.ni
        vyema TFF na vyama vya mikoa kwa kupitia utaratibu wa PPP (Public Private
        Sector Partnership) vikaingia ubia na wamiliki wa viwanja hivi ili TFF na
        washirika wake wachukue jukumu la kuviboresha,kuvisimamia na kuviendesha ili
        kuhakikisha vinakuwa katika viwango stahili kwa mujibu wa kanuni za FIFA na
        CAF.Hii itaongeza usalama wa wachezaji na watazamaji na kuinua mapato
        yatokanayo na viwanja hivi
        Ushiriki wa wadau
        Kwa sasa taswira ya mpira wa miguu inawafungia nje wadau wengi ambao kama wangepewa fursa
        ya kushiriki nao wangetaka wachangie maendeleo ya mpira wa miguu.Juhudi kubwa inabidi zitumike
        kurudisha imani hii ili kuleta hisia za umoja wa kitaifa katika kuendesha mpira wetu (sense of
        belongingness) .Ni muhimu taasisi muhimu za kitaifa zishirikishwe katika sekta hii ya mpira wa
        miguu ,hii ni pamoja na taasisi kama Tacaids,Mashirika ya utalii kama TANAPA na TTB,Umoja wa
        wafanyabiashara kama TPSF,CTI na TCCIA ,Kituo cha uwekezaji TIC n.k.Ushirikiano huu utasaidia
        kujenga jina la Tanzania pale tunapoandaa michuano ya kimataifa na pia kuhamasisha vijana wetu
        waepuke maisha hatarishi kama vile kujihusisha na ngono isiyokuwa salama,madawa ya kulewa
        (kutumia na kusafirisha),ulevi wa kupindukia n.k.
        HITIMISHO
        Ndugu zangu,nihitimishe kwa kusisitiza kuwa maendeleo ya mpira Tanzania kwa hapa
        yalipofikia yanahitaji ubunifu,ujasiri na msukumo mpya ili tuweze kuunyanyua mpira wetu na
        kuupa mwelekeo mpya,mwelekeo wa matumaini ,mwelekeo wa kulipeleka soka letu katika
        kushinda vikombe vikubwa barani mwetu Afrika na Duniani.
        Shime wapiga kura nipeni fursa hii ya kuwa Rais wa TFF ili kwa pamoja tukishirikiana na
        wadau wote muhimu katika sekta yetu tuweze kulisikuma gurudumu hili ili hatimae soka iweze
        kuiletea nchi yetu sifa na kuwapa raha mamilioni ya watanzania wapenda mpira.
        Pamoja tutaweza
        Chagua MALINZI
        Chagua MABADILIKO
        Mungu ibariki Afrika
        Mungu ibariki Tanzania
        Jamal Malinzi
        Mgombea nafasi ya Urais
        TFF
        2013
        Mpira ni afya, mpira ni burudani, mpira ni ajira kwa vijana!
        MAELEZO BINAFSI YA JAMAL EMIL MALINZI MGOMBEA URAIS TFF
        Tarehe ya kuzaliwa : 08 Agosti, 1960
        Elimu: 1974-1977 : Sekondari O-Level
        Mwanza Secondary School
        1978-1981 : A-Level
        Ilboru High School
        1980-1981 : JKT – Ruvu
        Operesheni TIJA
        1981-1985 : Chuo Kikuu Dar Es Salaam
        Digrii ya Uhandisi (Upper 2nd Class)
        1986-1993 : Ajira -Coopers and Lybrand
        Tanzania Industrial Research
        and Development Organization
        1993-Hadi Leo : Mjasiriamali
        Mkurugenzi – Cargostars Limited
        Michezo : Nimekuwa promota wa mchezo wa ngumi za kulipwa
        kuanzia kipindi cha 1995-2001. Baadhi ya mabondia
        wangu walifikia kiwango cha kimataifa hadi kusaini
        mkataba na Promota maarufu duniani Don King.
        : Nimekuwa Seneta wa Yanga na baadae nikawa
        Mkurugenzi na mwisho nikawa Katibu Mkuu wa Klabu
        ya Yanga kati ya mwaka 1999 na 2005.
        : Nimekuwa Mkurugenzi na Msimamizi Mkuu wa Timu ya
        Mkoa wa Dar Es Salaam ya Mzizima United. Timu hii
        ndiyo ya mwisho kushinda Kombe la Taifa mwaka 2007
        ikiwa timu moja ya Mkoa wa Dar Es Salaam.
        : Nimekuwa mjumbe wa Baraza la michezo la mkoa wa
        Dar es salaam 2009-2011
        : Nimekuwa Mwenyekiti wa kamati ya mashindano mkoa
        wa Pwani 2009-2011
        : Hadi sasa mimi ni mwenyekiti wa Chama cha mpira wa
        miguu mkoa wa Kagera
        : Kikampuni, Kampuni yetu ya Cargostars Limited ina
        uzoefu wa muda mrefu wa kudhamini michezo
        mbalimbali. Kwa kipindi cha miaka saba Cargostars
        Limited iliidhamini mbio za marathon za wabunge.
        Aidha Cargostars Limited ina rekodi ya kudhamini
        michezo mingine kadhaa ikiwemo mpira wa miguu,
        ngumi, Tennis na Golf,".
        • Blogger Comments
        • Facebook Comments

        0 comments:

        Item Reviewed: MALINZI AZINDUA KAMPENI ZA KURITHI KITI CHA TENGA TFF LEO, AAHIDI MAMBO MAKUBWA SOKA YA TANZANIA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry