Wednesday, June 13, 2012

    UNAMKUMBUKA MARIO ALBERTO KEMPES?


    Kempes enzi zake

    WENGI wanaamini vipaji vya wanasoka wa zamani huwezi kuviona katika dunia ya leo, hasa upande wa washambuliaji, ingawa wanasoka wa siku hizi wanavuna fedha nyingi kuliko wakali wa enzi hizo.
    Vyombo vya habari vinawapamba sana, lakini bado wapembuzi yakinifu wanaamini hawawezi kufanya mambo kama yaliyowahi kufanywa na magwiji wa enzi hizo.
    Lionel Messi ni mzuri na ndiye mwanasoka bora wa dunia, lakini kumbuka vitu vya Diego Maradona na toa jibu la swali; nani mkali kati ya Waargentina hao?
    Kutoka taifa hilo hilo wanalotoka wakali hao wawili, amewahi kutokea mwanasoka mwingine mkali ambaye dunia haipaswi kumsahau, huyo si mwingine zaidi ya Mario Alberto Kempes.
    Mkali huyo alizaliwa Julai 15, 1954 Bell Ville, Córdoba, ni mwanasoka wa zamani wa Argentina. Baba yake Mario naye alikuwa mchezaji, hivyo alimvutia kucheza soka kuanzia akiwa mdogo. Akiwa na miaka saba, alianza kucheza soka katika timu za watoto na alipotimiza miaka 14 alijiunga na klabu ya La Cuarta de Talleres. Alijipatia umaarufu zaidi alipochezea klabu ya Valencia na kuwa sehemu muhimu ya kikosi cha Argentina kilichoshinda michuano ya Kombe la Dunia mwaka 1978.
    Kempes alikuwa na majina ya utani kama El toro na El Matador. Katika kipindi chake cha kwanza na Valencia alishinda tuzo ya ufungaji bora kwa kufunga mabao 24 msimu wa 1976-77 na mabao 28 msimu wa 1977-78. Maisha yake ya soka yalianzia katika klabu ya mjini kwao ya Instituto kabla ya kujiunga na Rosario Central, ambako alifunga mabao 85 katika mechi 105, akidhihirisha kwamba yeye ni mfungaji mbao wa hatari, jambo lililomsaidia ajiunge na Valencia, akiwa Valencia alishinda taji la Copa del Rey, Kombe la Washindi barani Ulaya na taji la UEFA Super Cup. Alikuwa akijulikana na kwa tabia yake ya kujituma zaidi awapo uwanjani, alikuwa na tabia ya kupiga mashuti akiwa nje ya eneo la hatari pia uwezo wa kukimbia na mpira kuingia golini, na hakuwa na hakuwa na tabia kama washambuliaji wengine ya kukaa ndani ya eneo la hatari bali alikuwa akizunguka kila upande. Wengi walikuwa wakipata tabu sana kumkaba kutokana na staili yake ya uchezaji.
    Kempes akishangilia moja ya mabao yake enzi zake
    Kabla ya Kombe la Dunia la mwaka 1978, Kempes alikuwa ndio mchezaji pekee wa Argentina aliyekuwa akicheza nje ya nchi katika kikosi Kocha César Luis Menotti, kipindi hicho alikuwa akicheza Hispania katika klabu ya Valencia wakati wachezaji wengine wote katika kikosi cha Argentina walikuwa wakicheza nyumbani. Kocha alimuelezea wakati akitaja kikosi kwa ajili ya michuano ya Kombe la Dunia la mwaka 1978 kwa kusema, “Ana nguvu, uwezo wa kuchezea mpira, anajua kutengeneza nafasi na anapiga mashuti makali. Ni mchezaji atakayeongeza kitu katika kikosi na anaweza kucheza kama mshambuliaji wa kati.”
    Wakati akiitwa kwenye kikosi cha timu hiyo, Kempes alikuwa ametoka kuwa mfungaji bora katika ligi kuu ya Hispania (La Liga) kwenye misimu miwili iliyopita na alikuwa amedhamiria kuwaonyesha mashabiki wa soka wa nchi yake kwamba anaweza kufanya makubwa kwenye michuano mikubwa ya soka ulimwenguni. Hata hivyo, mwaka 1974, akiwa na umri wa miaka 20 alishindwa kufunga bao hata moja kwenye michuano hiyo iliyofanyika Ujerumani Magharibi na hata baada ya mechi za hatua ya makundi kumalizika katika michuano ya Mwaka 1978 alikuwa bado hajafunga bao hata moja katika michuano hiyo.
    Katika maisha yake ya soka alifanikiwa kuichezea Argentina katika michezo 43 na kufunga mabao 20. aliiwakilisha nchi yake katika michuano mitatu ya Kombe la Dunia ile ya mwaka 1974, 1978 na 1982, na kuafanikiwa kushinda michuano hiyo mwaka 1978 huku akifunga mabao sita katika michuano hiyo yakiwemo mawili katika mechi ya fainali. Pia aliwahi kufunga mabao muhimu katika maisha yake ya soka ngazi ya kimataifa.
    Mwaka 1978 alishinda tuzo ya Mchezaji bora wa mwaka wa Marekani Kusini, utoaji wa tuzo hiyo ulifanyikia Caracas, Venezuela. Alitajwa katika orodha ya Pele ya wachezaji bora 125 ambao bado wapo hai Machi 2004.
    Kempes wa sasa
    Kempes alianza kufundisha soka kwa mara ya kwanza nchini Albania. Wakati akifundisha klabu ya Lushnja ya Albania aliweka rekodi ya kuwa kocha wa kwanza wa kigeni kusajili mchezaji wa kigeni katika historia ya soka la Albania. Maisha yake ya ukocha nchini Albania hayakuwa marefu yalifikia tamati mwaka 1997.  Mwaka uliofuata alipata kazi ya kufundisha klabu ya Mineros de Guayana ya Venezuela. Mwaka 1999, Kempes alihamia Bolivia na kufundisha klabu ya The Strongest, kabla ya kujiunga na klabu ya Blooming mwaka 2000. Kabla ya hapo aliwahi kufanya kazi kama kocha msaidizi wa Héctor Núñez katika klabu ya Valencia, pia aliwahi kuwa kocha mchezaji wa mabingwa wa Ligi Kuu ya Indonesia, Pelita Jaya. Alitangaza kustaafu soka mwaka 1996 akiwa na umri wa miaka 41.
    Kwa sasa anafanya kazi kama mchambuzi na mtangazaji wa soka katika kituo cha ESPN idhaa ya Kihispaniola. Huyo ndiye Mario Alberto Kempes, mtambo wa mabao ulioipa Argentina Kombe la Dunia mwaka 1978.

    WASIFU WAKE:
    JINA: Mario Alberto Kempes
    KUZALIWA: Julai 15, 1954 (Miaka 56)
    ALIPOZALIWA: Argentina
    NAFASI: Mshambuliaji
    TIMU ALIZOCHEZEA:
    Mwaka            Timu
    1970–1973      Instituto (Mechi 13, mabao11)
    1974–1976      Rosario Central (Mechi 107, mabao 85)
    1977–1981      Valencia (Mechi 142, mabao 95)
    1981–1982      River Plate (Mechi 29, mabao 15)
    1982–1984      Valencia (Mechi 42, mabao 21)
    1984–1986      Hércules (Mechi 38, mabao 10)
    1986–1987      First Vienna (Mechi 20, mabao 7)
    1987–1990      St. Pölten (Mechi 64, mabao 24)
    1990–1992      Kremser SC (Mechi 39, mabao 7)
    1995                Fernandez Vial (Mechi 11, mabao 5)
    1996                Pelita Jaya  
    (Tangu mwaka 1973 hadi 1982, aliichezea Argentina mechi 43 na kuifungia mabao 20)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: UNAMKUMBUKA MARIO ALBERTO KEMPES? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry