// Disable text selection (not fully reliable) function disableSelection(element) { element.setAttribute('unselectable', 'on'); element.style.userSelect = 'none'; element.style.MozUserSelect = 'none'; element.style.webkitUserSelect = 'none'; } // Apply to the entire document body document.addEventListener('DOMContentLoaded', function() { disableSelection(document.body); }); MTIBWA SUGAR YENYE SIFA ZA BARCELONA - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE MTIBWA SUGAR YENYE SIFA ZA BARCELONA - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE
    Wednesday, May 16, 2012

    MTIBWA SUGAR YENYE SIFA ZA BARCELONA


    Hussein Javu katikati kwenye mazoezi wa Stars, akiwatoka Ramadhan Chombo kushoto na Juma Nyosso kulia



    Mtibwa, mabingwa wa Tusker 2009

    Nizar Khalfan
    BARCELONA ya Hispania pamoja na kusifiwa kuwa klabu yenye mafanikio makubwa na kutandaza soka safi kwa sasa- lakini pia ina sifa moja ya ziada ambayo ni kuwa klabu inayozalisha wachezaji wengi bora.
    Hata katika wakati ambao Barcelona ilikuwa haiwiki kwenye soka duniani, bado iliendelea kuzalisha wachezaji bora waliochukuliwa na klabu kubwa Ulaya wakiwa makinda- mfano Fabregas aliyekwenda Arsenal.  
    Hata Tanzania kuna klabu ambayo unaweza ukaibebesha sifa za Barcelona, nayo ni Mtibwa Sugar ya Morogoro.
    Wachezaji wengi walio kwenye klabu kubwa Tanzania ama waliibuliwa Mtibwa au walipitia chuo cha mafunzo, Manungu mfano kwenye kikosi cha mabingwa wa Ligi Kuu, Simba SC utakutana na Juma Kaseja, Amir Maftah, Uhuru Suleiman, Salum Machaku na Obadia Mungusa.
    Yanga pale utakutana na Kiggi Makasy, Pius Kisambale, Kiggi Makassy, Shaaban Kado na Julius Mrope, wakati Azam, FC wanaye Deo Munishi ‘Dida’.
    Bado hujamtaja kiungo Nizar Khalfan, aliyechezea klabu za Vancouver Whitecaps na Philadelphia Union za Marekani, au Idrisa Rajab anayekipiga Sofapaka ya Kenya.
    Unaizungumzia klabu yenye maskani yake kjijiji cha Madizini, tarafa ya Turiani, Wilaya ya Mvomero, kiasi cha kilomita 100 kutoka Morogoro mjini, ambayo ilianzishwa mwaka 1988 na kikundi cha wafanyakazi wa kiwanda cha sukari cha Mtibwa, Mtibwa Sugar Estates Ltd.
    Timu hiyo ilianza kushiriki Ligi ya Wilaya Daraja la Nne mwaka 1989 na iliendelea vizuri hadi kupanda Daraja la Kwanza 1996, ambayo mwaka 1998 ilibadilishwa na kuwa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.
    Mwaka 1998, kiwanda hicho kilinunuliwa na kampuni ya Tanzania Sugar Industry, ambao waliifanya klabu hiyo kuwa tishio, wakianza kwa kufanya usajili wa kishindo, wakichukua nyota wa klabu za Simba na Yanga.
    Kado
    Monja Liseki, Yussuf Macho, Mwanamtwa Kihwelo, Ally Yussuf ‘Tigana’, waliokuwa Yanga mwaka huo, Geofrey Kikumbizi aliyekuwa Majimaji walishuhudiwa msimu wa 1999 wakivaa jezi za Mtibwa. Mwishoni mwa msimu, Mtibwa iliwaongeza Duwa Said, Abdulmalik Nemes kutoka Simba, Kassim Issa aliyekuwa Zanzibar na Zuberi Katwila aliyerejea kutoka Ubelgiji kucheza soka ya kulipwa.
    Wakali hao waliungana na nyota walioipandisha Mtibwa kama Mecky Mexime, Hassan Mbarouk, Odo Nombo, Reuben Mgaza, Kassim Mwabuda, Mao Mkami ‘Ball Dancer’, Vincent Peter, Rajabu Msoma chini ya kocha John Simkoko. 
    Mtibwa Sugar ambayo kwa sasa inafundishwa na Mkenya, Thom Olaba, imekuwa na sera ya kuinua vipaji, ambavyo baadaye vinapapatikiwa na klabu kongwe za Simba na Yanga.
    Lakini zaidi, Mtibwa ina mchango mkubwa katika timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, kwani imekuwa ikitoa wachezaji wengi kwa ajili ya timu hiyo.
    Mtibwa Sugar, inayojulikana kwa jina la utani kama Wakata Miwa wa Manungu, ni miongoni mwa klabu chache nchini zinazojivunia mafanikio ambayo siri yake ni uongozi bora na mfumo bora wa utawala.
    Lengo la Mtibwa ni kuwa timu imara na yenye mafanikio zaidi kutoka ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati.
    Na kwa sababu hiyo, wakati wote Mtibwa imekuwa yenye maandalizi mazuri chini ya makocha wa viwango vya juu. Mafanikio ya Mtibwa Sugar hadi sasa ni kuwa timu ya tatu kutoka nje ya Dar es Salaam kuwahi kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwa misimu miwili mfululizo, 1999 na 2000.
    Kaseja
    Hiyo ni timu pekee nje ya Simba na Yanga kuwahi kutetea ubingwa wa Ligi Kuu, ingawa kwa sasa cheche zake zimefifia.
    “Unajua wakati ule tulikuja kwa kishindo sana, hadi tukaitwa Magalactico (Real Madrid) wa Manungu, lakini ule ulikuwa ni mwanzo tu ili kutafuta namna ya kupata mashabiki. Ila baada ya hapo sera yetu imekuwa kuinua vipaji.
    Na tunashukuru kwa asilimia 80 tumefanikiwa. Karibu kila msimu tunauza wachezaji si chini ya wawili kwenda Simba na Yanga. Msimu huo uliomalizika pia, SImba walichukua wachezaji wawili kwetu, Salum Machaku na Obadia Mungusa, Yanga nao waliwachukua Mrope na Kado.
    Bado kuna wachezaji wetu waliong’ara msimu huu ambao hizo klabu zinawatolea macho mfano Juma Abdul na Hussein Javu. Wote hawa wanatoka timu ya vijana ya Mtibwa katika mradi wetu wa soka ya vijana, ambao ni imara sana. Tunasikitika vyombo vya habari haviuzungumzii, labda kwa sababu tupo kijijini kule, lakini mbona matunda yake yanaonekana?”anasema Mratibu wa Mtibwa Sugar, Jamal Bayser katika mahojioano na BIN ZUBEIRY leo mchana ofisini kwake, Superdoll, barabara ya Nyerere, zamani Pugu, Dar es Salaam.
    Tangu watwae ubingwa wa Ligi Kuu mara mbili mfululizo, Mtibwa imekuwa timu tishio katika soka ya Tanzania na inavipasua kichwa haswa vigogo, Simba na Yanga. Haijawahi kutetereka, licha ya kusajili wachezaji mahiri, kuwa na mpango mzuri wa kuinua chipukizi, pia imekuwa ikiajiri makocha wa kigeni.
    Miongoni mwa makocha wa kigeni waliowahi kufanya kazi Manungu ni Raoul Shungu, raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Olaba, Twahir Muhiddin na James Siang’a kutoka Kenya.
    Mwaka 2009, Mtibwa Sugar ambayo ni timu nyingine yenye Uwanja wake, Manungu baada ya Azam na Yanga inayomiliki ‘Uwanja mbovu’ wa Kaunda, ilitwaa Kombe la Tusker, linaloshirikisha timu za Afrika Mashariki na mwaka juzi ilitwaa Ngao ya Jamii baada ya kuifunga Yanga 2-1. 
    Lakini cheche za Mtibwa zimefifia, Bayser anasemaje? “Fitina zimezidi katika soka hii, rushwa imetawala mno, sisi hatuwezi kuhonga, tunataka kushinda kwa uwezo. Kwa mfano msimu huu ulioisha dhamira yetu ilikuwa ubingwa, ila soka ya nchi hii imeharibika mno hivi sasa,”anasema.
    Hata hivyo, Bayser aliyewahi kuwa Makamu wa pili wa rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) katika awamu ya kwanza ya Utawala wa Leodegar Chilla Tenga, anasema wanajipanga na wanaachana na sera za Arsene Wenger za kuuza wachezaji bora wa timu. “Hatuuzi mchezaji tena, tunataka ubingwa msimu ujao, tutahakikisha kila mchezaji tunayemuhitaji haondoki ili aisaidie timu.
    Tayari Javu ambaye alikuwa amemaliza Mkataba, tumemuongezea ili kuhakikisha haondoki,”anasema Bayser. Hao ndio Mtibwa ambao wana sifa za Barcelona, mabingwa wa soka wa dunia.    
    Jamal Bayser kulia, akiwa na Ofisa mwenzake wa kampuni ya Superdoll na sanamu ya Michellin, moja ya bidhaa za kampuni yao, kampuni tanzu ya Mtibwa Sugar.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTIBWA SUGAR YENYE SIFA ZA BARCELONA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry