Kikosi cha Yanga |
TIMU za Simba na Yanga za Dar es Salaam leo zinaingia kwenye
viwanja tofauti katika mfululizo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, baada ya mwishoni
mwa wiki kushindwa kung’ara.
Yanga itaingia Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kucheza na
African Lyon ikijaribu kujisafisha baada ya Jumamosi kufungwa mabao 3-1 na Azam
kwenye uwanja huohuo, huku Simba ikiwa ugenini Uwanja wa Jamhuri, Dodoma kuivaa
Polisi ya mjini humo.
Yanga inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi ikiwa
na pointi 37 kwa michezo 19, huku Azam ikishika nafasi ya pili ikiwa na pointi
41 sawa na Simba inayoongoza ligi hiyo ikiwa pia na pointi 41, lakini ina
uwiano mzuri wa mabao ya kufunga.
Mchezo wa Yanga na African Lyon unatarajiwa kuwa wa vuta
nikuvute kutokana na Yanga kuwa na hasira ya kufungwa na Azam, hivyo itataka
ishinde ikae sawa kwenye msimamo wa ligi.
Lakini Lyon nayo haipo pazuri kwenye msimamo wa ligi, ikiwa
nafasi ya kumi kwenye msimamo kati ya timu 14 zinazoshiriki ligi hiyo baada ya
kujikusanyia pointi 18 kwa michezo 18.
Hivyo ni wazi mchezo huo utakuwa wa vuta nikuvute kwani Lyon
sasa itakuwa inapigania kutoka kwenye ukanda wa kushuka daraja, huku Yanga
ikipambana kuhakikisha inapunguza pengo lake la pointi na vinara wa ligi hiyo.
Kwa upande wa Simba baada ya Jumapili kutoka 0-0 na Toto
Africans ya Mwanza inayoshika nafasi ya pili kutoka mkiani, leo itacheza na
Polisi inayoshika nafasi ya mwisho mkiani.
Lakini Polisi licha ya kuburuza mkia ikiwa na pointi 14 kwa
michezo 19, imekuwa ikiisumbua Simba mara kwa mara zinapokutana, hivyo ni wazi
mchezo wa leo utakuwa na ushindani wa aina yake.
0 comments:
Post a Comment