KOCHA Arsene Wenger amepongeza "ujasiri"
uliooneshwa na kikosi chake na hatimaye kufanikiwa kupata ushindi dakika ya
mwisho ya mchezo dhidi ya Newcastle.
Hii ni mara ya nne kwa vijana wa Arsenal kuanza kufungwa
katika michezo ya Ligi Kuu ya England na hatimaye kuibuka washindi, wakati
katika pambano dhidi ya Newcastle alikuwa Thomas Vermaelen aliyeipatia ushindi
Arsenal baada ya kuunganisha viziri mpira wa pembeni wa Theo Walcott.
Wenger amesema: "Kilichofanya tuwafunge ni ujasiri
wetu."
"Sikutarajia kama tutashinda. Nilikuwa nlimwambia
msaidizi wangu tunahitaji kushambulia mara moja zaidi na tutafunga."
Arsenal walikuwa nyuma ya Tottenham kwa pointi 10 katika mbio
za kuwania nafasi ya tatu, kabla ya pambano lao mwezi uliopita, lakini Gunners
kwa sasa wapo nyuma ya majirani wao hao kwa pointi moja tu baada ya kuendeleza
ushindi katika mechi zao zilizopita.
Kikosi hicho cha Wenger kilianza kufungwa katika uwanja wa
Emirates Stadium katika mechi ya nne mfululizo wakati Hatem Ben Arfa alipoachia
mkwaju pembeni mwa nguzo ya lango, lakini Robin van Persie alijibu kwa kishindo
ndani ya dakika moja tu na kuandika bao lake la 44 katika mechi 45 za Ligi Kuu
ya England, kabla Vermaelen kuipatia Arsenal bao la ushindi dakika ya mwisho ya
mchezo.
"Hii ilikuwa ni mechi muhimu kwa timu zote,"
alisema Wenger.
"Newcastle ni timu nzuri na unahitaji kitu maalum kuweza
kuwalaza."
Newcastle walijaribu kutupunguza kasi lakini tulifanikiwa
kuwapenya mara nyingi. Tulipata dakika tano za nyongeza na hizo zilitusaidia
kushinda.
"Tulishinda katika dakika ya mwisho dhidi ya Sunderland,
Liverpool na sasa Newcastle. Hii inaonesha tunadhamira ya ushindi.
Walcott - ambaye alicheza kwa kiwango cha juu katika muda
wote wa mchezo - anaamini timu yao inaweza kuwaengua Tottenham katika nafasi ya
tatu.
"Tottenham hawana budi kujitazama upya sasa,"
alisema Walcott.
"Kutokana na kikosi tulichonacho na tukiwa na wachezaji
wengi ambao wanarejea baada ya kuumia, tunaamini tutaweza kufika mbali zaidi.
"Umekuwa ni msimu wa kukurukakara nyingi za kufanya
vizuri na kuporomoka, lakini namna unavyomaliza ndio jambo la muhimu
zaidi."
Kwa upande wake meneja wa Newcastle Alan Pardew anahisi kikosi
chake kilistahili kupata angalao pointi moja, lakini aliwataka wachezaji wake
wasihuzunike sana kwa kupoteza mchezo hali itakayopunguza matumaini yao ya
kucheza soka ya Ulaya.
Newcastle wapo nyuma kwa pointi tano dhidi ya Chelsea
wanaoshikilia nafasi ya tano zikiwa zimesalia mechi 10 kabla msimu
haujamalizika.
"Kilikuwa ni kibarua kigumu," Pardew aliongeza.
"Tumecheza na kikosi ambacho kiwango chake kimeimarika
na ari yao iko juu. Tulijaribu kuwazuia wasicheze mchezo wao kwa muda mrefu na
walituweka katika wakati mgumu.
"Kusema ukweli imetuumiza sana. Timu kubwa huwa
zinafunga mabao dakika za mwisho. Kwa ujumla usiku huu tulistahili pointi moja.
"Tunakabiliwa na mchezo mgumu siku ya Jumamosi dhidi ya
Norwich na tunahitaji kushinda, kwa hiyo tunahitajika kuhakikisha
tunajitengeneza upya."
0 comments:
Post a Comment