Ligi Kuu ya Vodacom inaingia raundi ya 21
kesho (Machi 14 mwaka huu) kwa mechi mbili ambapo mabingwa watetezi Yanga
watakuwa nyumbani kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuikabili African
Lyon.
Viingilio katika mechi hiyo
itakayoanza saa 10.30 jioni ni sh. 3,000 viti vya bluu na kijani, sh. 5,000 viti
vya rangi ya chungwa, sh. 10,000 kwa VIP C na B wakati VIP A itakuwa sh.
15,000.
Mechi nyingine ya kesho
itachezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma ambapo Simba watakuwa wageni wa
timu ya Polisi Dodoma.
Yanga itarejea tena uwanjani Machi 17 mwaka
huu kwa pambano dhidi ya wenyeji Villa Squad litakalofanyika Uwanja wa Chamazi,
Dar es Salaam wakati siku hiyo hiyo Coastal Union itacheza na Oljoro JKT kwenye
Uwanja wa Mkwakwani, jijini Tanga.
Machi 18 mwaka huu kutakuwa
na mechi tatu ambapo Simba itakuwa ugenini Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro
dhidi ya Mtibwa Sugar, Toto African itaikaribisha Polisi Dodoma jijini Mwanza
wakati Azam na Ruvu Shooting Stars zitaoneshana kazi kwenye Uwanja wa
Chamazi.
TEMEKE UTD, SMALL KIDS KUSHUSHANA MACHI
31
Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa
Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana Dar es Salaam jana (Machi 12 mwaka huu) imeamua
timu za daraja la kwanza za Temeke United na Small Kids zicheze mechi Machi 31
mwaka huu mjini Dodoma ili kupata moja itakayoshuka daraja.
Kwa mujibu wa Kanuni ya 4 ya
Ligi Daraja la Kwanza timu tatu zitashuka daraja, moja kutoka katika kila kundi.
Kwa vile AFC ya Arusha na Manyoni ya Singida kutoka kundi C tayari zimeshashuka,
Kamati ya Ligi imeamua Temeke United na Small Kids zilizoshika nafasi ya mwisho
katika makundi yao ya A na B zicheze mechi hiyo ili kupata moja itakayokamilisha
idadi ya timu tatu za kushuka daraja.
Baada ya kumalizika hatua ya
kwanza ya Ligi Daraja la Kwanza, timu tisa zimefanikiwa kucheza hatua ya fainali
ya Tisa Bora na nyingine tano za Burkina Faso ya Morogoro, Morani ya Manyara,
Polisi ya Iringa, Majimaji ya Songea na Green Warriors (94KJ) zimefanikiwa
kubaki Ligi Daraja la Kwanza.
0 comments:
Post a Comment