// Disable text selection (not fully reliable) function disableSelection(element) { element.setAttribute('unselectable', 'on'); element.style.userSelect = 'none'; element.style.MozUserSelect = 'none'; element.style.webkitUserSelect = 'none'; } // Apply to the entire document body document.addEventListener('DOMContentLoaded', function() { disableSelection(document.body); }); RAMADHAN SULEIMAN CHOMBO: - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE RAMADHAN SULEIMAN CHOMBO: - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE
  • HABARI MPYA

    Saturday, March 17, 2012

    RAMADHAN SULEIMAN CHOMBO:


    KWA nini Redondo? Ni soka yake maridadi tangu akiwa kinda, akicheza chandimu kwenye vichochoro vya mitaa ya Keko Magurumbasi, wilayani Temeke, Dar es Salaam ilimfanya afananishwe na kiungo wa zamani wa kimataifa wa Argentina, Fernando Carlos Redondo Neri.
    Leo anacheza Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, lakini ni kinyume kabisa cha ndoto zake, kwa nini?
    “Bila kurudishwa nchini kwa kukosa kibali sasa hivi ningekuwa Norway nacheza mpira, ” anasema Ramadhan Suleiman Chombo ‘Redondo’ katika mahojiano na DIMBA wiki hii.
    Kiungo huyo ambaye alikuwemo kwenye kikosi cha timu ya Tanzania Bara ‘Kilimanjaro kilichokuwa kinashiriki michuano ya CECAFA Tusker Challenge, anasema ataendelea kucheza kwa kujituma katika timu yake ya Azam FC ili aone faida ya mpira  hapo baadaye.
    “Wengi wanapenda kusema kuwa ndoto zao za baadaye ni kuwa mchezaji wa kulipwa, hilo sikatai hata mimi napenda kuwa hivyo, lakini pia nataka kuona mpira utanipa nini katika maisha yangu hasa nitakapostaafu kucheza,” anasema Redondo.
    Akielezea historia yake ya soka, Redondo anayemudu kucheza nafasi ya kiungo na winga kulia na kushoto, anasema anakumbuka ilikuwa ni mwaka 2000 alipokuwa kwenye kituo cha Dar es Salaam Youth Olimpic Centre, wakati huo timu yao ilienda Sweden kwenye mashindano ya vijana.
    “Wakati huo ndio nilikuwa natoka kumaliza elimu yangu ya msingi, nilishindwa kuendelea na masomo kwani nilikuwa napenda sana mpira hivyo ningeshindwa kusoma, baada ya kumaliza eilimu ya msingi timu yetu ilikwenda Sweden, bahati nzuri tukatwaa ubingwa wa Gothia nchini humo baada ya kuwafunga Rusia katika fainali,” anasema
    Kiungo huyo anasema michuano hiyo iliyokuwa ikishirikisha nchi  mbalimbali yalijulikana kama Gothia, na timu yao ilikuwa ni tishio sana kwa nchi mbalimbali zilizoshiriki michuano hiyo na bahati nzuri wakachukua ubingwa.
    Redondo ambaye wiki iliyopita alisherehekea siku yake ya kuzaliwa sambamba na sherehe za miaka 50 ya Uhuru (Redondo alizaliwa Desemba 9 mwaka 1987, anasema anakumbuka ilikuwa mwaka 2002 wakati timu yao ya vijana Dar es Salaam Youth Olimpic Centre ilipokwenda kwenye michuano mingine nchini Norway, anasema aliwahi kuzamia nchini humo.
    “Nilizamia Norway kuanzia mwaka 2003 hadi 2007 nilikuwa nikichezea timu ya Lyngdal iliyokuwa ikishiriki daraja ya pili nchini humo, bahati mbaya katika msako ikabainika kwamba sina kibali cha kuishi nchini humo, hivyo nikarudishwa hapa Tanzania,” anasema
    Anasema alirudi nchini mwanzoni mwa  mwaka 2007, baada ya kutoka Norway akawa anacheza Ligi ya TFF kinondoni katika timu ya Tambaza, mwaka huo huo akajiunga na timu ya Ashanti United iliyokuwa ikishiriki Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara ambayo alicheza nusu msimu na 2008 akasajiliwa na Simba.
    “Unajua mpira ni malengo na ili uwe mchezaji mzuri ni lazima ufuate misingi bora ya soka, hapo ndipo utakapotimiza ndoto zako, hasa kama unajua kuwa mpira ndio ajira yako ya kudumu,” anasema.
    Redondo anasema alidumu katika timu ya Simba tangu 2008 hadi 2010 aliposajiliwa na Azam FC ambayo ndio anaichezea hadi sasa.
    Katika siku ambazo Redondo anasema hata kuja kusahau katika maisha yake ni pale alipopata ajali ya pikipiki siku ya Simba Day, anasema alikuwa akitokea kambini siku hiyo walikuwa wanacheza na timu ya URA ya Uganda.
    “Ilikuwa ni mwaka 2008 siku ya Simba Day na mimi nilipanga kuonyesha vitu adimu katika mechi yetu na URA, lakini bahati mbaya sikuweza kucheza na tulifungwa na timu hiyo bao 1-0, siku hiyo huwa siisahau maishani mwangu,” anasema.
    Redondo anasema alikaa nyumbani mwezi mmoja kwani aliumia kiuno hivyo daktari akamtaka apumzike mwezi mzima kwa ajili ya matibabu ndio arejee tena uwanjani.
    Anaishauri nini TFF?
    “Wawe na maandalizi ya muda mrefu kwa timu  pindi yanapokaribia mashindano mbalimbali kwani itasaidia kuwa na timu nzuri ya kiushindani, mbali na hilo pia wazisaidie klabu zinazoshiriki Ligi Kuu ili ziweze kupata wadhamini kwani kuna timu ambazo hazina wafadhili na zimekuwa zikishindwa kujiendesha zenyewe,” anasema.
    Anasema TFF wajaribu kuongea na makampuni mbalimbali ili yaweze kuzisaidia timu ambazo hazina uwezo, kwani nyingi zinashindwa kuleta upinzani kwa saababu hazina uwezo.
    “Kila siku tutakuwa tukishuhudia upinzani kwa timu za Simba, Yanga, Azam FC na zile za majeshi kwa kuwa ndizo zinazoweza kujiendesha, na ili soka liwe na ushindani mkali timu hizi ambazo hazina wafadhili zitafutiwe ili ligi iwe na upinzani kwa kila timu,” anasema.
    Akizungumzia matatizo ambayo wachezaji wengi wamekuwa wakikumbana nayo, anasema kwanza kabisa ni viwanja, anasema mikoa mingi viwanja vyao ni vibovu hivyo wanapotakiwa kucheza mechi mikoani huwa wanakumbana na tatizo hilo.
    “Pia utakuta mechi ni keshokutwa, timu inasafiri leo kutoka Dar es Salaam kwenda Bukoba tena kwa basi, hivyo mchezaji akifika anakuwa amechoka na safari na hata uwanjani hawezi kujituma vizuri,” anasema.
    Redondo anasema lakini kuna timu ambazo zinauwezo kama kuna mechi sehemu ya mbali wanapanda ndege hivyo hata akifika anakokwenda hawezi kuwa na uchovu kama yule aliyepanda basi.
    Wachezaji ambao Redondo anasema wanamvutia kwa hata Tanzania ni viungo Haruna Niyonzima, Haruna Moshi ‘Boban’ Mwinyi Kazimoto na Nurdin Bakari.
    “Wapo wengi zaidi ya hao, lakini hao ndio nawapa nafasi kubwa kwa hapa Tanzania,” anasema.

    WASIFU WAKE:
    JINA: Ramadhan Suleiman Chombo
    JINA LA UTANI: Redondo
    KUZALIWA: Desemba 9, 1987 (miaka 24)
    ALIPOZALIWA: Dar es Salaam
    NAFASI: Kiungo/winga
    KLABU YAKE: Azam FC
    Mwaka                 Klabu
    2000-2002                       DSM Youth Olimpic Centre (kituo)
    2003-2006                       Lyngdal (Norway)
    2007                    Ashanti United
    2008-2010           Simba
    Tangu 2010:         Azam FC
      
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: RAMADHAN SULEIMAN CHOMBO: Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top