// Disable text selection (not fully reliable) function disableSelection(element) { element.setAttribute('unselectable', 'on'); element.style.userSelect = 'none'; element.style.MozUserSelect = 'none'; element.style.webkitUserSelect = 'none'; } // Apply to the entire document body document.addEventListener('DOMContentLoaded', function() { disableSelection(document.body); }); MWANAHAMISI OMARY SHARUWA: - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE MWANAHAMISI OMARY SHARUWA: - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE
  • HABARI MPYA

    Saturday, March 17, 2012

    MWANAHAMISI OMARY SHARUWA:


    “MWANAMKE kucheza mpira watu wasichukulie kama ni uhuni, ni kazi kama zilivyo kazi nyingine, na mimi sitarudi nyuma, nitazidi kusonga mbele zaidi”.
    Ndivyo alivyoanza kuzungumza, mshambuliaji wa timu ya taifa ya wanawake Tanzania, Twiga Stars, Mwanahamisi Omary Sharuwa, ambaye pia anachezea klabu ya Mburahati Queens.
    Mwanahamisi, aliyepachikwa jina Gaucho kutokana na uchezaji wake, akifananishwa na mwanasoka bora wa zamani wa dunia, Ronaldinho Gaucho, ni mchezaji tegemeo wa Mburahati Queens na timu ya taifa, na labda ni maradhi tu yanayoweza kumuweka nje ya kikosi cha kwanza cha Twiga, au Mburahati.
    Uwezo mkubwa wa kusakata kandanda alionao mshambuliaji huyo wa Mburahati Queens na Twiga Stars, Mwanahamisi Omary uliwahi kuzua utata Machi mwaka jana, katika mechi ya Ligi ya wanawake   Dar es Salaam iliyofanyika kwenye Uwanja wa Karume na kushuhudia Mwanahamisi akifunga mabao saba peke yake na kuiwezesha Mburahati Queens kushinda mabao 10-1 dhidi ya Uzuri Queens.
    Uwezo wake mkubwa wa kupiga chenga, kasi na kufunga mabao zaidi ya matatu katika kila mechi aliyokuwa akicheza katika ligi hiyo, uliwafanya mashabiki wanaofika uwanjani hapo kushuhudia soka la wanawake kudai kuwa huenda mchezaji huyo ana jinsia mbili na kwamba yawezekana kuwa jinsia ya kiume ndiyo yenye nguvu zaidi hivyo kumfananisha na mwanariadha mahiri nchini Afrika Kusini, Caster Semenya.
    Katika tukio ambalo halitakuja kusahaulika  kwa mashabiki wa kandanda nchini, ni pale mchezaji huyu alipokuwa ni mmoja wa wafungaji wa bao kati ya mawili waliyoifunga Namibia katika kampeni za kusaka tiketi za kufuzu kwa fainali za wanawake za Afrika.
    Wakiwa ugenini huko Windhoek nchini Namibia, timu ya Taifa ya wanawake ya Twiga Stars iliweza kuondoka na pointi zote tatu muhimu baada ya kuwachapa wenyeji wao kwa mabao 2-0. Huku wakicheza kwa kujiamini na umahiri mkubwa, kinadada hao wa Tanzania waliweza kujiweka vyema kwenye duru ya kwenda kucheza fainali ya Mataifa ya Afrika kwa upande wa wanawake, bao lingine lilifungwa na Asha Rashid, maarufu kama Mwalala.
    Katika mahojiano yake maalumu aliyoyafanya na DIMBA hivi karibuni, Mwanahamisi ‘Gaucho’ anasema hakuna kitu ambacho kinamsikitisha kwa baadhi ya mashabiki kuchukulia soka la wanawake kama uhuni.
    “Mimi nasema naomba mashabiki waone mpira kwa wanawake ni kitu  cha kawaida, nchi nyingi za wenzetu zinauthamini sana mpira wa wanawake, hivyo na Tanzania inatakiwa tuuige utamaduni huo.
    “Wengine huwa wanatuona kama madume, jamani sisi wanawake kama wengine ni mpira tu ndio unaotufanya tuwe hivi, lakini hakuna kitu kingine chochote, mpira kwetu ni kama jeshini tu, kwani jeshini watu wote ni sawa,” anasema Gaucho.
    Gaucho aliyezaliwa mwaka 1992 mkoani Tanga na kupata elimu yake ya msingi Pangani Tanga, anasema alianza kupenda soka tangu akiwa shuleni, na hata alipomaliza masomo yake ya msingi, moja kwa moja akajikita katika soka.
    “Nakumbuka nilikuja Dar es Salaam kwa mama yangu mdogo na baba mdogo, siku hiyo nikaenda kuangalia mechi za wanawake katika Uwanja wa Benjamini Mkapa, nilipoiona timu ya Mburahati Queens nikavutiwa nayo.
    “Baada ya mchezo wao kumalizika nikazungumza na kocha wao, ambaye aliniomba niungane nao, wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 15 tu, lakini uwezo niliokuwa nao ulimvutia sana kocha wangu, hivyo akaniweka katika kikosi cha kwanza,” anasema.
    Anasema siku za mwanzo alipojiingiza katika soka, walezi wake walimkataza kucheza, lakini yeye akawa anajiiba hivyo hivyo, wazazi wa Gaucho wote wawili walifariki, hivyo akawa analelewa na mama yake mdogo na baba mdogo.
    “Nilikuwa nikijiiba tu kucheza, kwa kweli mwanzo ulikuwa mgumu, lakini baadaye ilibidi waniachie tu, kwani waligundua kuwa nilikuwa nikicheza kwa kificho, lakini kwa sasa wananipa ushirikiano mkubwa, hivyo baada ya kufanya mazoezi na Mburahati Queens kwa kificho hatimaye nikasajiliwa rasmi,” anasema.
    Anasema tangu siku hiyo akawa mchezaji wa Mburahati Queens, wakati huo ilikuwa ni mwaka 2003, na akiwa katika timu hiyo ndani ya mwaka huo akaitwa kwenye timu ya taifa akiwa na umri huo huo wa miaka 15, huku wenzake wakiwa na umri mkubwa kidogo.
    Baada ya kuitwa katika timu ya taifa, anasema aliongeza bidii uwanjani na ndio maana hadi leo makocha wamekuwa wakimtegemea katika kikosi cha kwanza katika timu yake ya taifa na klabu yake ya Mburahati Queens.
    Anasema malengo yake katika soka ni kufika mbali, lakini wasiwasi wake ni kwamba ndoto zake zitashindwa kutimia kwa kuwa timu nyingi za wanawake hazina wafadhili, kitu ambacho kinawaangusha.
    “Sio katika klabu tu kwani hata timu yetu ya taifa haina wafadhili zaidi ya kuwategemea TFF tu (Shirikisho la Soka Tanzania), lakini kama wangekuwa na wafadhili wangefika mbali sana,” anasema.
    Gaucho atakumbukwa kwa mengi  hata katika michuano ya Shirikisho la Soka Kusini mwa Afrika (COSAFA).
    Katika mechi yao na Botswana iliyochezwa kwenye Uwanja wa Gwanzura jijini Harare, Zimbabwe, Twiga walishinda mabao 3-1 na waliong’arisha mechi hiyo alikuwa ni Gaucho aliyetupia nyavuni mabao 2 na Fatuma Mustafa ‘Kitu Nini’ alifunga moja.
    Pia katika michuano hiyo Twiga walipocheza na Afrika Kusini, walitoa sare ya mabao 2-2, na aliyesawazisha bao la pili ni Gaucho, ni mchezaji ambaye ana uchu na mabao pindi timu yake inapocheza.
    Pia Mei mwaka 2010 timu hiyo ilipokuwa ikicheza mchezo wa kutafuta tiketi ya kufuzu kwa fainali za Mataifa ya Afrika kwa wanawake, iliwahi kutoa kipigo cha mbwa mwizi kwa Eritrea mabao 8-1, kati ya mabao hayo Gaucho alifunga manne. Akizungumzia mechi yao ya marudiano dhidi ya Namibia itakayochezwa Dar es Salaam leo, Gaucho anasema kama waliweza kushinda ugenini, bila shaka hata nyumbani wataleta raha, na kwa kushirikiana na wachezaji wenzake anaamini hilo litawezekana.
    “Muhimu ni mashabiki kujitokeza kwa wingi uwanjani ili kutupa sapoti, kwani ugenini tulicheza tukiwa wakiwa, hivyo mechi ya marudiano tunaomba sapoti kutoka kwa Watanzania,” anasema.
    Twiga inahitaji hata sare leo ili kusonga mbele katika kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Mataifa ya Afrika kwa Wanawake, kwani katika mchezo wa kwanza ilishinda 2-0 ugenini.
    Wachezaji wanaomvutia kwa Tanzania ni Mrisho Ngassa wa Azam FC na Cristiano Ronaldo wa Real Madrid ya Hispania.
    Katika tukio ambalo anasema hatakuja kusahau katika maisha yake, ni mwaka 2003 alipoitwa katika timu ya taifa  ya wanawake, Twiga Stars, kwani alikuwa na umri mdogo sana wa miaka 15, hivyo kwake lilikuwa ni tukio la aina yake.
    “Tukio hilo kwangu huwa ni la kukumbukwa sana, kwani sikuwahi kuota kama ipo siku nikiwa na umri mdogo kama ule ningeitwa kwenye timu ya taifa,” anasema.
    Gaucho amewaomba watu wenye uwezo wazisaidie na timu za soka za wanawake, kama ilivyo kwa timu za kiume, anaamini kama watapata wafadhili watafika mbali sana, na watatoa burudani nzuri sana kwa mashabiki wa soka nchini.
    Kuhusu maisha yake binafsi, Gaucho huyo wa Mburahati anasema kwamba hana mume wala mtoto, lakini ana rafiki wa kiume, ambaye hata hivyo anasema hataki kumuanika- hiyo ni siri yake na huyo ni mwandani wake.
    Naam, huyo ndiye Mwanahamisi Omary Sharuwa au Gaucho, binti wa Mburahati anayeibeba Twiga Stars kwenye michuano ya kimataifa.
    Je, leo ataendelea kung’ara na jezi za bendera ya nchi? Bila shaka hilo ni jambo la kusubiri na kuona jinsi mambo yatakavyokuwa pale Taifa.

    WASIFU WAKE:
    JINA: Mwanahamisi Omary Shuruwa
    KUZALIWA: Desemba 12, 1992 (miaka 20)
    ALIPOZALIWA: Tanga
    KLABU YAKE: Mburahati Queen
    KLABU ALIZOCHEZEA:
    Mwaka           Klabu
    2003               Mburahati Queen

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MWANAHAMISI OMARY SHARUWA: Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top