VIONGOZI wa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara,
kesho watakuwa na kikao kizito mjini Dar es Salaam, kujadili ‘changa la macho’
walilopigwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Habari za ndani ambazo bongostaz imezipata kutoka kwa umoja
wa klabu za VPL, zimesema kwamba kikao hicho kinafuatia TFF kuwahadaa kuhusu
suala la kampuni ya Ligi Kuu.
Kiongozi mmoja wa klabu, ameiambia bongostaz leo kwamba Kamati
ya Ligi Kuu iliyoundwa na TFF haikuwasilisha hoja ya Kampuni katika kikao cha
Kamati ya Utendaji kilichofanyika Februari 12, mwaka huu.
Kiongozi huyo, alisema mtu ambaye anaingia kwenye Kamati ya
Utendaji ya TFF kutoka kwenye Kamati yao ni Mwenyekiti wao pekee, Wallace Karia.
“Karia pekee ndiye Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF
ambaye kutoka kwenye Kamati ya Ligi Kuu iliyoundwa na TFF anaingia kwenye kikao
cha Kamati ya Utendaji.
Lakini ajabu, habari ambazo tumezipata ni kwamba
hajawasilisha hoja hiyo na hakuna mtu aliyeinuka kuhoji kuhusu suala la kampuni,”
alisema kiongozi huyo.
Kiongozi huyo, alimlalamikia rais wa TFF pia, Leodegar
Chillah Tenga kwamba aliziahidi klabu yeye mwenyewe atasimamia hadi kuhakikisha
suala la kampuni linaingia kwenye Kamati ya Utendaji, lakini ajabu ameendesha
kikao cha Kamati ya Utendaji bila kujadili kampuni.
“Mbaya zaidi ni kwamba, sasa wanakwenda kwenye Mkutano Mkuu
(utakaohusisha uchaguzi Mkuu pia) bila ajenda ya kampuni,” alilalamika kiongozi
huyo.
Akiizungumzia Kamati ya Ligi Kuu, kiongozi huyo alisema
kwamba ipo kama kivuli na haihusiki na uendeshaji wa Ligi Kuu
“Karia anaishi nje ya Dar es Salaam, Ofisa waliyesema
ataajiriwa, hadi leo hajaajiriwa. Kazi zote zinafanywa na ofisi ya Sadi Kawemba
kama zamani,”alisema.
Kamati ya Ligi Kuu inaundwa na Wallace Karia (Mwenyekiti),
Said Mohamed (Makamu Mwenyekiti), Damas Ndumbaro, Yahya Ahmed, Meja Charles
Mbuge, Steven Mguto, Geoffrey ‘Kaburu’ Nyange, Seif Ahmed, Kamishna Msaidizi wa
Polisi, Hemedi Msangi na Henry Kabera (Wajumbe).
0 comments:
Post a Comment