// Disable text selection (not fully reliable) function disableSelection(element) { element.setAttribute('unselectable', 'on'); element.style.userSelect = 'none'; element.style.MozUserSelect = 'none'; element.style.webkitUserSelect = 'none'; } // Apply to the entire document body document.addEventListener('DOMContentLoaded', function() { disableSelection(document.body); }); DAVIES ROBBY MWAPE - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE DAVIES ROBBY MWAPE - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE
  • HABARI MPYA

    Wednesday, March 14, 2012

    DAVIES ROBBY MWAPE


    Mwape katika mechi na El Merreikh ya Sudan Julai mwaka jana
    Mwape na familia yake
    ALITUA Yanga katika dirisha dogo la usajili wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara msimu uliopita, lakini kufika Oktoba mwaka jana zikaanza tetesi kwamba, Davies Robby Mwape anaweza kuachwa katika dirisha dogo la usajili wa Yanga msimu huu.
    Kwa nini? Kuumia mara kwa mara, kuliwafanya viongozi wa klabu hiyo wahisi mchezaji huyo amefikia ukingoni kisoka, lakini dakika 90 za mchezo uliopita wa Ligi Kuu dhidi ya watani wa jadi, Simba zilitosha kumnusuru Mzambia huyo kutupiwa virago Jangwani.
    Mwape aliifunga bao pekee la ushindi Yanga katika dakika ya 72, baada ya kutumia vizuri makosa ya safu ya ulinzi ya ulinzi ya Simba.
    Victor Costa alipiga mpira ili kuuondosha kwenye hatari, lakini ukamgonga Juma Said Nyosso, ambaye alizubaa ‘kuuongezea safari’ hadi Mwape akauwahi na Juma Kaseja alipotoka langoni, akamrahisishia kazi Mzambia huyo kwa kufunga bao hilo.
    Mwape alikuwa nje ya Uwanja wakati Yanga inafungwa 2-0 na mahasimu wao hao katika mechi ya Ngao ya Jamii, Agosti 17, mwaka jana, kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya misuli, lakini Oktoba 31, mwaka jana alikuwa bora na kudhihirisha umuhimu wake kwenye mechi za watani wa jadi.
    Machi 5, 2011 Mwape alikuwa anaelekea kufunga bao katika mechi ya marudiano ya Ligi Kuu dhidi ya Simba, lakini beki Juma Nyosso akamkwatua kwenye eneo la hatari na refa Orden Mbaga akaamuru ipigwe penalti, iliyokwamishwa kimiani na Stefano Mwasyika dakika ya 59, kabla ya Mussa Hassan Mgosi kuisawazishia Simba dakika ya 73.
    Hata hivyo, wakati Yanga ipo katika maandalizi ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu, mshambuliaji huyo ameshindwa kuwasili kujiunga na wenzake.
    Nini kinaendelea? Mwape anasema hayuko fiti kwa asilimia 100, ila haumwi wala si majeruhi. Uongozi wa Yanga unasema Mwape amebaki kwao anajitibu na amepewa ruhusa na uongozi.
    Anajitibu nini ikiwa haumwi? Ipo siri kubwa ambayo pande zote mbili zinaificha na itakuwa vigumu yeyote kujua bila ya wahusika kufunguka.

    MWAPE NI NANI?
    Davies Robby Mwape, mshambuliaji aliyesajiliwa kutoka Konkola Blades ya Zambia, ambaye kusajiliwa kwake Yanga kulitokana na kufahamiana kwake na kocha wa Yanga, Kostadin Bozidar Papic ambaye aliwahi kufanya naye kazi Afrika Kusini.
    Lakini ni mwandishi mmoja wa habari alimuunganisha tena Mwape na Papic baada ya kupotena. “Rafiki yangu mmoja mwandishi wa habari hapa Tanzania alinitaarifu kama Papic ananitafuta na sasa yuko Yanga, kwa kuwa Papic alikuwa kocha wangu wakati nacheza Orlando Pirates, nikakubali, akaniunganisha naye hatimaye mpango ukafanikiwa na nikaja Yanga,” anasema.

    Mwape na uzoefu wa mechi za watani wa jadi?
    “Nina uzoefu wa kucheza katika timu yenye mpinzani wa jadi, nimekuwa Orlando Prates, ni wapinzani wa Kaizer Chiefs, katika msimu wangu mmoja tu nilifunga bao la ushindi kwenye fainali ya Vodacom Challenge tukishinda 2-1.  
    Soka ni mchezo wa nafasi, nimekutana na Simba na nikapata nafasi, nikawafung. Nakumbuka nilipowafunga bao Kaizer Chiefs wakati nipo Pirates, mashabiki walifurahi sana, walishangilia kwa sababu yangu, nilifurahi sana, kuwafunga wapinzani wa jadi ni raha sana… nataka niendelee kufanya hivyo tena na tena nikiwa Yanga,”anasema Mwape.
    Mwape anazungumzia fainali za Kombe la Dunia zilizopita Afrika Kusini, ambako pamoja na Afrika kuwa weneyeji walishindwa kufika angalau Nusu Fainali kwa kusema kwamba; “Watu weupe wametuzidi sana, wana kila kitu. Afrika tuna timu, lakini tunahitaji kukaa na timu ya taifa kwa muda mrefu kambini tucheze pamoja tuzoeane. Drogba akiwa Ivory Coast hawezi kucheza kama anavyocheza Chelsea, lakini kama timu zitaweza kuwa na wachezaji angalau kwa miezi miwili mfululizo kambini wakifanya mazoezi pamoja, tunaweza kusogea mbele,”anasema.
    Mwape anavutiwa na mchezaji gani duniani? “Nampenda Ronaldo Lima,”anamtaja mpachika mabao wa zamani wa kimataifa wa Brazil.
    Katika kucheza kwake kote soka, mabao mengi zaidi alifunga akiwa Chambishi SC ya Zambia ikimenyana na National Assembly mwaka 2004, alipiga matatu peke yake, lakini anasema zaidi amekuwa akifunga hadi mabao mawili kwenye mechi moja.
    Mwape ni mshambuliaji wa staili gani? “Staili yangu ni bull dozer (kunyanyasa mabeki), kasi, kutumia nguvu, kupiga mashuti, vichwa, Yanga wanaona wenyewe kazi yangu, nitaendelea kupigana kwa uwezo wangu wote,”anasema.
    Davies Robby Mwape alizaliwa Desemba 5, mwaka 1986, Kitwe, Zambia na alipata elimu ya Msingi katika shule ya Kawama na sekondari alisoma Mindolo, hadi Kidato cha Tano, zote zipo Kitwe.
    Kisoka, Mwape kama walivyo nyota wengi duniani, alianzia utotoni kabisa akicheza timu ya watoto ya Police Tigers, iliyokuwa inaundwa na vijana wa umri chini ya miaka 14, mwaka 2003 akasajiliwa na timu ya Daraja la Kwanza, Kwiza FC aliyoichezea kwa msimu mmoja tu, kabla ya kuhamia Chambishi FC ya Ligi Kuu mwaka 2004.
    Akiwa Chambishi mwaka 2004, Mwape anasema aliunganishiwa nafasi ya kwenda kufanya majaribio Ufaransa katika klabu ya Chateroux na mshambuliaji wa zamani wa kimataifa wa Zambia, Kalusha Bwalya na akafuzu na kupewa mkataba wa miaka minne.
    Hata hivyo, pamoja na uongozi wa Chateroux kumtajia mkataba utakavyokuwa ikiwemo mishahara posho na kadhalika, Mwape anasema siku moja akaambiwa chukua barua hii mpelekee Bwalya Zambia.
    “Nikapanda ndege kurudi Zambia, sikuifungua ile barua kufika nikampa Kalusha, akaniambia atanitafuta. Hakuwahi kunitafuta tena, ndio nikapata nafasi nyingine Pirates. Lakini baadaye nikagundua FAZ walitaka fedha nyingi sana kutoka Chateroux, wakaghairi,”anasema Mwape. 
    Hata hivyo, anasema hajakata tamaa ya kucheza Ulaya anaamini kama atafanikiwa kufanya vizuri Yanga kuanzia ligi ya nyumbani hadi michuano ya Afrika, anaweza kupata nafasi ya kurejea Ulaya.
    Mwape anasema alidumu Orlando Pirates tangu 2005 hadi 2006 alipohamia Jomo Cosmos
    “Pirates walinitoa kwa mkopo kwenda klabu moja inaitwa FC AK, nilienda lakini sikucheza, kwa sababu hakukuwa na nafasi ya mchezaji wa kigeni, walikuwa wana wageni watano tayari, wakawa wanasubri mchezaji mmoja apate uraia ili wanisajili mimi…ndio nikaamua kwenda Jomo,”anasema.
    Alidumu Jomo Cosmos hadi mwaka 2009 aliporejea Zambia kujiunga na Zanaco, kufuatia mkataba wake kumalizika nchini humo.
    Kwa nini alitemwa Jomo Cosmos? “Afrika Kusini wamepitisha sera ya kutosajili wachezaji wa kigeni ili kukuza uwezo wa wachezaji wao. Wachezaji wengi wameondolewa kwenye timu Afria Kusini na wamekimbilia timu ndogo ndogo ambazo hata maslahi yako chini,”anasema Mwape, ambaye kutoka Zanaco, alijiunga na Power Dynamos alikocheza nusu msimu na kujiunga na Konkola Blades ambako baada ya miezi kadhaa, akatua Yanga.
    Mwape ana mchango wake katika tiketi ya Zambia ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2006 nchini Misiri, kwani alicheza mechi zote za kuwania kufuzu chini ya kocha Kalusha Bwalya, lakini anasema timu ilipofuzu akaumia na kuwa nje ya kikosi.
    “Nimechezea timu ya taifa mwaka 2005 na 2006 chini ya Kalusha. Nilicheza mechi za kufuzu 2006, timu ilipofuzu nikaumia, sikwenda Misri, tangu nimepona sijapata nafasi tena.
    Mwape ni mume wa Lucia waliyefunga naye pingu za maisha mwaka 2005 na wamefanikiwa kupata mtoto mmoja aitwaye Richard, ambaye ana umri wa miaka sita sasa. Je, atapenda mwanawe acheze soka pia? “Sitaki kuingilia uhuru wa mwanangu, ataamua yeye mwenyewe kuhusu maisha yake,”anasema Mwape, ambaye familia yake ipo Kitwe.
    Baba yake, Robby Mwape ni Mhandisi, wakati mama yake Lwini Soneka alifariki dunia Januari mwaka juzi mjini Kitwe.
    Mwape ana kaka yake aitwaye William Soneka Mwape ambaye aliwahi kucheza soka katika nafasi ya kiungo kwenye klabu ya Kitwe United.
    Huyo ndiye Davies Robby Mwape, mshambuliaji ambaye hajaripoti kambini kwa maandalizi ya mzunguko wa pili wa Ligi na Ligi ya Mabingwa, ambayo Yanga itaanza na Zamalek ya Misri.
    Je, kuna nini kinaendelea juu yake na klabu yake? Dar es Salaam, Yanga wanasema anaumwa, yeye anazungumza kutoka Zambia anasema yupo fiti kabisa. Yetu macho na masikio, tuvute subira. Tutajua ukweli.   


    WASIFU WAKE:
    JINA: Davies Robby Mwape
    KUZALIWA: Desemba 5, 1986
    ALIPOZALIWA: Kitwe, Zambia
    KLABU YAKE: Yanga
    KLABU ALIZOCHEZEA:
    2004-2005: Chambishi FC (Zambia)
    2005-2006: Orlando Pirates (A. Kusini)
    2006-2009: Jomo Cosmos (A. Kusini)
    2009:           Zanaco (Zambia)
    2010:          Power Dynamos (Zambia)
    2010:          Konkola Blades (Zambia)


    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DAVIES ROBBY MWAPE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top