// Disable text selection (not fully reliable) function disableSelection(element) { element.setAttribute('unselectable', 'on'); element.style.userSelect = 'none'; element.style.MozUserSelect = 'none'; element.style.webkitUserSelect = 'none'; } // Apply to the entire document body document.addEventListener('DOMContentLoaded', function() { disableSelection(document.body); }); ABDALLAH AHMED BIN KLEB: - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE ABDALLAH AHMED BIN KLEB: - BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE
  • HABARI MPYA

    Wednesday, March 14, 2012

    ABDALLAH AHMED BIN KLEB:


    Bin Kleb akimkabidhi jezi Niyonzima
    BAADA ya Yussuf Mehboob Manji, kutangaza kujivua ufadhili wa klabu ya Yanga ya Dar es Salaam, wapenzi wa klabu hiyo waliingiwa hofu kidogo juu ya mustakabali wa klabu yao.
    Hali ilikuwa mbaya kati ya 2003 hadi 2006 alipojitokeza Manji na kuwekeza fedha nyingi kwenye klabu hiyo, hata ikaweza kurejesha hadhi yake, kusajili wachezaji wa gharama na kuwa mshindani wa kweli.
    Lakini hofu iliyotanda kwa kuondoka Manji, imezimwa na wapenzi kadhaa wa Yanga, waliounda umoja wao na kuamua kwa hali na mali kuusaidia uongozi wa klabu hiyo katika masuala mazito ya klabu, kama usajili, maandalizi, malezi ya wachezaji na kadhalika.
    Ni orodha ndefu kidogo, lakini DIMBA imefanikiwa kukutana na mmoja wa wanachama hao ‘waliochizika’ na Yanga, ambaye amechoma mamilioni yake kibao kuisaidia klabu hiyo.
    Huyo ni Abdallah Ahmed Bin Kleb, mfanyabishara kijana ambaye mtandao wake wa kibiashara umeenea Afrika Mashariki na Kati. Moja kati ya mambo ambayo kwa sasa wana Yanga wanafurahia ni mataji mawili mfululizo, ubingwa wa Bara na Kombe la Kagame pamoja na usajili ambao wao wanaamini ni mzuri.
    Katika mambo haya huwezi kumuweka kando Bin Kleb, kwani amechangia kwa kiasi kikubwa kufanikiwa kwake, akiwa Mjumbe wa Kamati ya Mashindano ya klabu chini ya Mwenyekiti Seif Ahmed na Mjumbe wa Kamati ya Usajili chini ya Mwenyekiti Salim Rupia.
    Katika mahojiano na DIMBA, Bin Kleb anasema kwamba yeye ni mpenzi wa Yanga tangu akiwa anasoma shule ya msingi, ingawa baba zake— mzazi na mdogo wote— ni Simba damu.
    “Mimi nilianza kuonyesha mapenzi yangu kwa Yanga tangu nikiwa mdogo sana, baba mdogo (Ali Bin Kleb) alikuwa mfadhili wa Simba wakati fulani, alikuwa ananichukua tunaingia na mabenz yetu Uwanja wa Taifa (sasa Uhuru), mimi nikishuka napanda jukwaa la Yanga, yeye anaenda la Simba.
    Hiyo ilikuwa ni miaka ya 1990, wapenzi wa Yanga walikuwa wanafurahi sana, basi nimeendelea kuwa Yanga hadi leo mimi ni mwanachama na kiongozi wa kamati mbili,”anasema.

    BIN KLEB NI NANI?
    Abdallah Ahmed Bin Kleb alizaliwa Septemba 2, mwaka 1973 katika hospitali ya Tumbi, Kibaha mkoani Pwani na alipata elimu yake ya msingi katika Shule ya Tumbi na Sekondari ya Forest Hill, Morogoro hadi Kidato cha Sita.
    Akiwa mtoto wa kwanza, katika familia yao, Abdallah alipomaliza Kidato cha Sita moja kwa moja alibeba majukumu ya kusimamia biashara za baba yake, jambo ambalo amelifanya kwa ufanisi kiasi cha kukuza biashara hizo za uuzaji mafuta, usafirishaji na utoaji mizigo bandarini.
    “Kwa kweli namshukuru Mungu sana, hivi sasa sisi ni miongoni mwa wafanyabiashara wanaofahamika nchi hii,”anasema Abdallah ambaye alisomea pia masomo ya biashara.

    BIN KLEB NA SOKA:
    Anasema soka alianza kuipenda tangu angali mdogo akiwa anasoma Shule ya Msingi na alikuwa akicheza winga ya kulia wakati huo hadi anafika sekondari.
    Anasema kwamba akiwa Kibaha pamoja na kuchezea timu ya Mwendapole FC alikuwa akiifadhili pia, lakini baadaye ukatokea mtafaruku akaenda kuanzisha timu yake mwenyewe, National FC.
    Anasema anakumbuka aliwahi hadi kumwalika mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Vaal Professionals ya Afrika Kusini, FC Zurich ya Uswisi, Stade Rennais, AS Monaco za Ufaransa, AS Roma ya Italia, Blackburn Rovers ya England na Galatasaray ya Uturuki, Nonda Shabani aichezee ‘ndondo’ timu yao hiyo.
    “Ilikuwa mwaka 1995, tulimualika Nonda na Monja (Liseki) wakati huo akiwa Sigara, waliichezea kwenye mashindano fulani hivi tukachukua Kombe, lakini timu haikudumu kutokana na mimi kujikita kwenye biashara,”anasema.
    Abdallah anasema kwamba lakini hadi leo anafanya mazoezi na kucheza mechi za maveterani, kwa kuwa soka ipo kwenye damu yake.

    BIN KLEB NA YANGA:
    Anasema alikuwa mpenzi wa kawaida tu wa Yanga miaka ya 1980 enzi hizo timu yao ikiundwa na wakali kama Ahmad Amasha, Charles Boniface Mkwasa, Juma Mkambi na wengineo, lakini baadaye akajikuta mapenzi yanazidi, kutokana na upinzani aliokuwa akiupata kutoka kwa wazazi wake.
    “Baba yangu mzazi na baba yangu mdogo walikuwa Simba sana, sasa ilikuwa Yanga ikifungwa wananitania sana, na mimi ndio nikaweka dhamira nikikua nikawa na kipato nitaisaidia Yanga, na kweli sasa hivi nasaidia timu ninayoipenda,”anasema.
    Anasema walianza kama wapenzi wa Yanga waliounda umoja wao kwa ajili ya kuisaidia timu yao chini ya uongozi wa Imani Madega, kwa kuchangishana fedha na kuwapa wachezaji au viongozi wahudumue timu.
    Anasema uongozi wa Lloyd Nchunga ulipoingia madarakani akateuliwa kwenye Kamati mbili, ya Mashindano na Usajili na anashukuru kazi zote amezifanya vizuri.
    “Tulianza kwa kuchukua Ngao ya Jamii tukiifunga Simba kwa penalti, tukaingia kwenye Ligi tukafanikiwa kuipokonya Simba ubingwa na juzi tumechukua Kombe la Kagame, tukiifunga Simba pia,”anasema.
    Abdallah anasema kwamba Novemba mwaka jana aliteuliwa kwenye Kamati ya timu ya taifa ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars na anashukuru pia huko aliiwezesha timu kutwaa ubingwa wa Challenge, kwa mara ya kwanza tangu itwae mara ya mwisho mwaka 1994.
    Anasema Yanga ingeweza kuwa mataji manne kwenye kabati lake mwaka huu kama si mgogoro baina ya Mwenyekiti wa klabu hiyo, Nchunga na Makamu wake, Davis Mosha kuiathiri timu hadi ikafungwa na Simba mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

    USAJILI BOMBA JANGWANI:
    Abdallah anazungumzia usajili wa Yanga msimu huu na kusema kwamba ni mzuri mno, kiasi kwamba anaweza kuufananisha na usajili wa mwaka 1994, kikosi kilichokuwa na wakali kama Riffat Said, Issa Athumani, Nico Bambaga, Method Mogella, Steven Mussa, Said Mwamba ‘Kizota’ (wote marehemu), Constantine Kimanda, Ngandou Ramadhan, Edibily Lunyamila, Mohamed Hussein, Sekilojo Chambua, Fumo Felician, Mtwa Kihwelo na wengineo.
    Kikosi anachojivunia Abdallah Bin Kleb msimu huu ambacho kimebeba Kombe la Kagame kwa mara ya kwanza tangu klabu hiyo itwae mara ya mwisho mwaka 1999 ni hiki; Yaw Berko, Nsajigwa Shadrack, Oscar Joshua, Chacha Marwa, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Juma Seif ‘Kijiko’, Godfrey Taita, Nurdin Bakari ‘Tshabalala’, Davies Mwape, Kenneth Asamoah, Kiggi Makassy, Bakari Mbegu, Rashid Gumbo, Julius Mrope, Jerry Tegete, Kiiza Hamisi, Shaaban Kado, Said Mohamed, Freddy Mbuna, Geoffrey Bonny, Haruna Niyonzima ‘Fabregas’, Pius Kisambale, Idrisa Rajab, Stefano Mwasyika, Abuu Ubwa, Shamte Ally, Job Ibrahim na Salum Telela.
    Anasema kikosi hiki kimeonyesha mwanzo mzuri kwa kutwaa Kombe la Kagame, kwani taji hilo lina maana kubwa Yanga.
    “Unajua Simba walikuwa wamechukua hilo Kombe mara sita, sasa kama wangechukua tena ingekuwa mara ya saba, ina maana wangezidi kutuacha mbali na kutukatisha tamaa, ila kuchukua kwetu ina maana katika rekodi wao wanatuzidi mara mbili tu sasa.
    Lengo letu ni kuhakikisha tunachukua tena na tena Kombe hilo hadi tuwafikie na kuwapita Simba kama tunavyowazidi kwenye Ligi ya Bara,”anasema.
    Anasema kutokana na kikosi hicho, wamedhamiria kutwaa ubingwa wa Bara na kufika hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani na ili kutimiza azma hiyo watahakikisha wanaiandaa vizuri timu na kuihudumia pia. 
    “Tumeweka kipaumbele katika suala la maslahi ya mchezaji, tutahakikisha kila mchezaji anatekelezewa haki zake zote za msingi zilizomo kwenye mkataba wake, sisi tunataka mataji tu,”anasema.

    USAJILI WA NIYONZIMA FABREGAS:
    Akizungumzia usajili wa Haruna Niyonzima ‘Fabregas’ kutoka APR ya Rwanda, Bin Kleb anasema kwamba baada ya kocha kupendekeza wachezaji anaowataka, Wajumbe wa Kamati ya Usajili waligawana majukumu, naye kwa kuwa ana ofisi zake Rwanda, akachukua jukumu la kumsajili mchezaji huyo.
    “Kocha alisema ni ngumu kumtoa Haruna APR, alikuwa haamini kabisa. Hata wajumbe wenzangu wa Kamati walikuwa hawaamini kabisa kama ninaweza kufanikisha hilo,”anasema.
    Bin Kleb anasema ‘aliingia kazini’ na hatimaye akafanikiwa kumpata Niyonzima na kumsainisha mkataba na ili kuwadhihirishia Wajumbe wenzake kwamba amefanikisha zoezi hilo pamoja na kuwatumia nakala za mkataba, pia aliwatumia picha akiwa na mchezaji huyo anasaini mkataba na kumkabidhi jezi namba nane ya Yanga.
    Hata hivyo, Bin Kleb anasikitika baada ya kusajiliwa mchezaji huyo, baadhi ya vyombo vya habari vimeibuka na maoni kwamba usajili wake haukutokana na ushauri wa kocha bali na maamuzi ya viongozi.
    “Huyu ni kati ya wachezaji ambao kocha alipendekeza wasajiliwe, hata wengine wote waliosajiliwa na kuachwa ni mapendekezo ya kocha. Kati ya wachezaji ambao kocha alipendekeza na tukawakosa ni Mussa Mgosi, Juma Kaseja, Obadia Mungusa na Mohamed Banka, yaani hawa wote wamo kwenye orodha ya kocha, sasa inakuwaje watu wanaibuka na maoni ya uongo?”anahoji Bin Kleb.
    Anasema maoni ya aina hiyo yanalenga kuwavuruga Yanga katika wakati huu na ameomba wapenzi wa klabu hiyo wayapuuze.

    UBABE WA YANGA KWA SIMBA:
    Bin Kleb anasema anafurahi kuwa sehemu ya mafanikio ya Yanga, kwani mbali na kutwaa mataji matatu, lakini wamemaliza msimu wakiwa wamewafunga wapinzani wao wa jadi, Simba mara tatu, kutoka sare moja na kufungwa moja.
    “Tuliwafunga katika Ngao, tukawafunga kwenye ligi mechi moja na kutoka sare moja, tumewafunga pia katika Kombe la Kagame, ni raha sana hii, wao walitufunga Kombe la Mapinduzi tu, tena kwa sababu tulikuwa tuna mgogoro, hatukujipanga vizuri,”anasema.
    Bin Kleb anasema kwamba matokeo ya Kombe la Mapinduzi yamemfundisha kwamba migogoro si mizuri katika klabu, hivyo amewataka wapenzi na wanachama wote wa Yanga kuhakikisha hawawi chanzo cha migogoro kwenye klabu hiyo.
    Aidha, anatoa wito kwa wana Yanga wote kwamba wasikae kusubiri klabu iwafanyie kitu, bali wanapaswa sasa kufikiria wataifanyia nini klabu yao.
    Ana ndoto za kuwa kiongozi wa Yanga siku moja? “Hapana, hapana kabisa, mimi nitaendelea kuwa nasaidia timu yangu tu, lakini uongozi hapana kabisa,”anasema.
    Naam, huyo ndiye Abdallah Ahmed Bin Kleb, mwanachama wa Yanga aliyefanikisha usajili wa Fabregas Jangwani.


    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ABDALLAH AHMED BIN KLEB: Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top